Buchosa. Siku moja baada ya aliyekuwa mwenyekiti wa Chadema Jimbo la Buchosa mkoani Mwanza Jaji Tasinga kukihama chama hicho na kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM) wanachama wa CCM wamepongeza hatua hiyo.
Akizungumza na Mwananchi leo Novemba 18, 2019 kada wa chama hicho, Samweli Kanizio amesema shukrani zote zimuendee Erick Shigongo kwa kutumia uwezo wake hadi Tasinga kurejea CCM kwenye chama chake cha zamani.
Amesema hata sisi wana CCM ilikuwa inatuuma Tasinga aliyekuwa mwenyekiti wa UVCCM kwa miaka kumi na mwenyekiti wa CCM wilaya ya Sengerema kwa miaka mitano halafu akahamia Chadema mwaka 2015.
"Tunamshukuru kurea kwake CCM, tuna imani upinzani tumeumaliza, tunachotakiwa wana CCM ni kumpatia ushirikiano wa dhati ili kumusaidia Mwenyekiti wa CCM Taifa John Magufuli," amesema Kanizio.
Diwani wa Chifunfu, Robert Madaha aliyewahi kuwa mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Sengerema na rafiki wa karibu wa Jaji Tasinga amesema fugisu ndani ya CCM ndizo zilimwondoa na kuhamia Chadema.
"Tunapaswa kudumisha umoja na mashikamano na siyo kurumbana kurudi kwake CCM Jaji Tasinga wengi wamefurahishwa lakini kuna baadhi ya wachache hawajafurahi kutokana na uchapakazi wake," amesema Madaha.
"Kada wa CCM Erick Shigongo anapaswa kupongezwa ndiye aliyemshawishi Jaji Tasinga kurejea CCM, makada kama hawa wanatakiwa kuthaminiwa kwa moyo wote ili kudumisha chama," amesema Kanizio.
Kwa upande wake, Tasinga amesema amewasamehe wote waliowaudhi akiwa CCM na waliomuudhi akiwa CCM anachowaomba washirikiane, wachapa kazi na CCM iendelee kudumu madarakani.