Arusha. Wakati joto la uchaguzi mdogo wa ubunge na udiwani likizidi kupanda, CCM wilaya ya Arusha kimependekeza majina ya madiwani wa Chadema waliohamia CCM kuwania nafasi za udiwani kupitia CCM.
Uchaguzi wa madiwani utafanyika Agosti 12 katika halmashauri 43 zilizopo mikoa 24 ya Tanzania Bara kutokana na baadhi ya madiwani kuhama vyama na wengine kufariki dunia.
Waliopendekezwa na CCM wilayani Arusha kuwania udiwani katika uchaguzi huo ni Prosper Msofe (Daraja Mbili),Elirehema Nko(Osunyai),Obeid Meng”oriki(Terat),Emmanuel Kessy(Kaloleni).
Madiwani waliopendekezwa na CCM kuwania udiwani katika uchaguzi mdogo walijiuzulu kwa nyakati tofauti jijini Arusha huku wakitaja hatua hiyo imetokana na kuunga mkono juhudi za Rais John Magufuli.
Akizungumza na gazeti hili leo Julai 10, akiwa ofisini kwake Katibu wa CCM wilayani Arusha,Musa Matoroka amesema fomu zilipelekwa katika ngazi ya kata kama utaratibu unavyoeleza na baadhi ya waliojitokeza ni madiwani waliojiuzulu Chadema.
Matoroka amesema mara baada ya kuyapokea majina hayo wameyapeleka kamati ya siasa ya mkoa kwa ajili ya kujadiliwa na kisha yatafikishwa mbele ya halmashauri kuu ya mkoa kwa ajili ya kupitishwa.