Dar es Salaam. Baadhi ya wakazi wa kata ya Vingunguti wamesema uwepo wa vituo vingi umesaidia kupunguza foleni wakati wa upigaji kura.
Wametoa kauli hiyo leo Jumapili Septemba 16, 2018 wakati wakizungumza na MCL Digital muda mfupi baada ya kupiga kura katika vituo mbalimbali.
Seleman Mgeni amesema utaratibu ni mzuri na watu hawakai muda mrefu katika foleni, anasema ukifika kituoni unatafuta jina na kuonyesha kitambulisho, kisha unaruhusiwa kupiga kura.
“Chaguzi zilizopita ukifika unaelezwa kuwa wazee wakae upande huu, ila uchaguzi wa leo hakuna hilo, ukipata maelekezo unakwenda katika chumba kutekeleza wajibu wako,” amesema Mgeni.
Melkion Ngimba ameungana na Mgeni kwa kusema utaratibu ni mzuri na hakuna usumbufu wowote.
“ Hadi sasa hali ni shwari, sijui kwa baadaye naomba Mungu mambo yaende hivihivi ili uchaguzi uwe huru na amani siyo hapa tu, bali na maeneo mengine," amesema Ngimba.