Dodoma. Wajane na wagane nchini Tanzania wametakiwa kujitokeza kuwania nafasi za uongozi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019 na si kubaki nyuma kwa sababu ya kufiwa na wenza wao.
Wametakiwa kutojiona wanyonge na kujifungia ndani, badala yake wachangamkie nafasi hizo.
Wito huo umetolewa na mkuu wa idara ya maendeleo ya wanawake Jinsia na Watoto katika Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Ruth Mbennah katika kongamano la tisa la kitaifa la wajane jijini Dodoma leo Jumatatu Septemba 16, 2019.
Kiongozi huyo amesema unyonge na huzuni umekuwa ukiwaponza kukosa nafasi nyingi za uongozi hata kama wana sifa au kupendwa na wananchi.
Amebainisha kuwa sasa ni wakati wa jamii kujua wajane na Wagane ni watu muhimu, licha ya kuondokewa na wenza wao haina maana wamepungukiwa uelewa.
Katibu wa CCT, mchungaji Canon Matonya amewataka wanandoa kujiandaa kisaikolojia kwa maelezo kuwa kati yao mmoja anaweza kutangulia mbele ya haki muda wowote.