Dodoma. Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, imeishauri Serikali kuwachukulia hatua za kinidhamu na za kisheria wale wote waliohusika kuingiza nchini Sulpher zaidi ya tani 400,000 zisizo na ubora na kusababisha madhara kwenye uzalishaji wa korosho.
Kauli hiyo imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk Christine Ishengoma leo Ijumaa Mei 17 2019, alipokuwa akiwasilisha maoni ya kamati kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2019/2020.
Lakini ameipongeza Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu (TOSC) na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kazi nzuri ya kuhakiki kudhibiti ubora wa pembejeo kwa kubaini kiasi hicho kisicho na ubora.
“Pamoja na kugundulika kwa pembejeo aina ya sulphur kukosa ubora, bado bei ya pembejeo hiyo imepanda kwa kasi kutoka Sh28,000 kwa msimu wa Korosho wa mwaka 2017/18 hadi kufikia Sh 60,000 kwa msimu wa korosho wa mwaka 2018/19,” amesema.
Amesema ongezeko hilo la bei na kwa kuzingatia kuwa msimu wa mwaka 2017/2018 kiuatilifu aina Sulphur kilitolewa bure kupitia fedha za export levy, inatazamiwa uzalishaji wa korosho utashuka kwa kasi kwa msimu wa 2019/2020.
Amesema bado kuna changamoto ya uwepo wa mbegu bandia inayochangiwa pamoja na mambo mengine upungufu wa watumishi hasa wakaguzi wa mbegu ikilinganishwa na mahitaji halisi.
Pia Soma
- Wafanyabiashara walia na kodi za mapato, upangishaji
- Heche ahoji kwa nini Serikali ya Tanzania imeshindwa na Gazeti la Kenya
- Mwenge wa Uhuru wazua jambo bungeni