Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA), wamelitaka Baraza la Mawaziri la nchi wanachama litazame suala la gharama za usafiri wa anga katika nchi wanachama kwa madai kuwa zipo juu.
Wameyasema hayo jijini Arusha wakijadili ripoti ya Kamati ya Hesabu ya Bunge hilo kwenye mkutano unaoendelea.
Mbunge wa bunge hilo kutoka Tanzania, Dk Abdulah Makame amesema taarifa ya kamati inaonesha kuwa gharama za usafiri wa ndege ndani ya nchi wanachama ni mara mbili ya bei kutoka nchi za EAC kwenda Dubai au Afrika Kusini.
Kwa mujibu wa Dk Makame, gharama zilizopo kwenye mfumo wa kodi na tozo zinazotozwa na mashirika ya ndege katika nchi za EAC ni kubwa.
Amesema ipo haja kwa Baraza la Mawaziri EAC kuboresha sera ya usafiri wa anga ili kuwapatia unafuu wananchi na wafanyabiashara.
Mbunge wa EALA kutoka Uganda, Kakooza James amesema gharama za usafiri wa ndege ndani ya jumuiya ni kikwazo, zinaumiza wananchi. Alipendekeza gharama za mashirika ya ndege katika nchi wanachama ziwe za aina moja.