Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Vijana wakumbushwa kuepuka rushwa Uchaguzi Mkuu

860cd3b6804a8295477aa1e0155a952d Vijana wakumbushwa kuepuka rushwa Uchaguzi Mkuu

Wed, 5 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

KUELEKEA uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu, vijana wametahadharishwa kutofanya makosa watakayojutia kwa kipindi cha miaka mitano ijayo kwa kuwachagua viongozi watoa rushwa.

Mchungaji wa Huduma ya Holyghost Fire International Miracle Centre, Idda Sirwa, alisema hayo alipokuwa akizungumza na vijana kwenye uzinduzi wa albamu ya mwimbaji wa nyimbo za Injili, Samweli Mwandoboka.

Sirwa akizungumza na vijana hao kwenye Kanisa la TAG, Mnadani Revival Temple Maili Mbili Dodoma alisema wakiwachagua viongozi hao kwa njia za rushwa watawagharimu.

Alisema kuwa wanaochaguliwa kwa njia ya rushwa watakaongoza nchi kwa maslahi yao binafsi kutokana na fedha na vitu mbalimbali walivyotoa kwa ajili ya kutaka kuchaguliwa.

“Hivyo ninawasihi vijana kote nchini kuhakikisha kwenye uchaguzi huu wa mwaka 2020 kujiepusha na kutokubali kudanganyika kwa rushwa ukizingatia kuwa itawagharimu,” alisema.

Kwa upande wake Mchungaji wa kanisa la TAG Mnadani, Marcel Mushi amewataka vijana kujikita kwenye shughuli mbalimbali za uzalishaji ili kuweza kujiinua kiuchumi. Alisema kuwa pamoja na kujihusisha na huduma mbalimbali za kiroho na kijamii, watumike pia kwenye uzalishaji ili wajikwamue na umaskini.

Naye Samweli Mwandoboka ambaye amezindua albamu yake amewataka vijana waliojiandikisha kwenye uchaguzi wa mwaka huu kutumia haki yao ya kimsingi kwa kujitokeza kupiga kura na kuwachagua viongozi wenye maadili na hofu ya Mungu.

Mwandoboka amewataka vijana hao kuhakikisha haki yao hiyo kuwachagua watakaofanya kazi na kumsaidia Rais Dk John Magufuli kwenye utendaji wenye maslahi ya kuwatumikia Watanzania bila kujali itikadi yoyote ya kidini na siasa.

Aliwataka vijana hao kutojihusisha na vitendo viovu, badala yake wajihusishe na ubunifu wa miradi huku wakimtumikia Mungu ili waweze kufanikiwa.

Chanzo: habarileo.co.tz