Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Vigogo Chadema wahitimisha kampeni Ukonga

17522 CADEMA+PIC TanzaniaWeb

Mon, 17 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Vigogo wa Chadema wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe wamehitimisha kampeni za ubunge Jimbo la Ukonga, huku wakijikita kuzungumzia uminywaji wa demokrasia na kumshukia mgombea wa CCM, Mwita Waitara.

 

Wengine waliokuwapo katika mkutano huo wa kampeni uliofanyika leo katika viwanja vya Mzambarauni ni Katibu Mkuu wa chama hicho, Vicent Mashinji na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye.

 

Wengine ni Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche, Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko; Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, Mbunge wa Bunda, Ester Bulaya; Mbunge wa Ndanda, Celil Mwambe na Mbunge wa Ukerewe, Joseph Mkundi.

 

Mbowe alisema kwa sasa kila Mtanzania ana hofu kutokana matukio yanayoendelea nchini ambayo yanafanyika kinyume na Katiba ya nchi, akitolea mfano kuwa vyama vya siasa vinaminywa.

 

Mbunge huyo wa Hai pia aligusia kuzuiwa kwa matangazo ya moja kwa moja ya Bunge akisema hoja iliyotolewa kuwa matangazo hayo yanasababisha watumishi wa Serikali kushindwa kufanya kazi  haina mashiko.

 

“Walizuia Bunge kwa kuwa walijua wakiruhusu mashine za upinzani kuzungumza pale bungeni wakiwamo wakina Sugu (Joseph Mbilinyi-Mbunge wa Mbeya Mjini), Matiko na Mdee wataibua madudu yao,” alisema.

 

Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, Sumaye alisema Jimbo la Ukonga lipo nyuma kimaendeleo na kugusia suala la elimu kuwa lengo si kutoa elimu bure bali kinachohitajika ni elimu yenye thamani.

 

Aliwataka wananchi kuendelea kulinda demokrasia kwa kuwachagua wabunge wa upinzani ili waisukume Serikali iwaletee maendeleo.

 

“Kama mnataka Mbunge wa kuwatetea basi ni Asia Msangi, mgombea ubunge wa Chadema Ukonga. Waitara (Mwita-mgombea wa CCM-Ukonga) akienda bungeni mdomo wake utakuwa umejaa maji na hataweza kuongea,” alisema.

 

“Waitara yeye atabaki kusema ‘ameonana na Rais tu’ na nyinyi wananchi hatawaona,” alisema.

 

Kwa upande wake, Dk Mashinji alisema CCM imechukua hoja ya Chadema ya kupinga rushwa. Alisema viongozi wa CCM wanahubiri kuwa rushwa imekwisha lakini ukweli ni kuwa rushwa imebadilishwa jina.

 

“Rushwa imebadilika kutoka kwenye kupeana vitu na sasa ni kupeana madaraka,” alisema.

 

“Mpeni kura Msangi kwa sera zake wala sio kwa kumuonea huruma. Mpeni kura ili kuonyesha kuwa wanawake wanaweza. Waitara anamnanga Asia kwa sababu ni mwanamke, hivi mimi mwanamke au mwanaume? Kama mimi mwanamke nimeweza na Asia ataweza mpeni kura,” alisema mzungumzaji mwingine Mdee.

 

Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Ilala, Dk Makongoro Mahanga aliwataka wananchi wa Ukonga kulinda kura zao.

Bulaya alisema Chadema ni chama kinachowaamini wanawake na hata yeye alisimamishwa kuwania ubunge na kuibuka mshindi.

 

“Mchagueni mwanamke kwa sababu akinamama hawafiki bei, hawanunuliki. Tuongezeeni nguvu bungeni kwa kumleta Asia,” alisema Matiko.

 

Uchaguzi mdogo wa ubunge Ukonga unafanyika kesho.

Chanzo: mwananchi.co.tz