Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Kamati Maalumu ya Uchaguzi wa Chama cha ACT- Wazalendo, Omar Said Shabaan amesema hatua inayofuata baada ya mchakato wa kuchukua na kurejesha fomu kukamilika ni mchujo wa wagombea utakaofanyika kati ya Machi Mosi na Machi 2.
Shabaan ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Februari 28, 2020 wakati akitoa taarifa ya mwenendo wa uchukuaji na urejeshaji fomu za kuwania nafasi ndani ya chama hicho ambao mchakato ulikamilika Februari 26 baada ya kudumu kwa mwezi mmoja.
"Zaidi ya wanachama 200 kutoka maeneo mbalimbali wamechukua na kurejesha fomu za kuomba uongozi ngazi mbalimbali. Kwa utaratibu wa kanuni za uchaguzi za chama majina haya yatapelekwa kwenye vikao vya uteuzi.
"Kikao cha kwanza kitakuwa ni Kamati Kuu kitakachoketi Machi Mosi na kuteua majina ya waliongea nafasi zote za ngome. Kutakuwa na kikao cha halmashauri kuu kitakachofanyika Machi 2 ambacho kitatea na kuchukua majina ya wagombea wote walioomba nafasi ya za kitaifa ndani ya chama hicho,"amesema Shabaan.
Shabaan amesema baada ya majina ya wagombea hao kupitia katika ngazi hizo kitakachofuata ni kampeni za watia nia hao zitakazodumu ndani ya siku saba.
Uchaguzi wa viongozi wakuu utafanyika Marchi 14, ukitanguliwa na chaguzi nyingine za ngome ya wazee, utakaofanyika Machi 7 na Machi 8 ngome ya wanawake.
Pia Soma
- Mwanyika wa Acacia na wenzake watimiza siku 498, gerezani bila upelelezi kukamilika
- Mahakama yazuia ndege kutoka China kuingia Kenya
- VIDEO: Askari aliyefukuzwa kazi kwa kumbaka mtoto wa askari apandishwa kizimbani
Ngome ya wanawake nafasi zinazogombewa ni mwenyekiti wa ngome, makamu mwenyekiti wa ngome, katibu na wajumbe wa halmashauri kuu(nafasi 15) na wajumbe wa kamati kuu (nafasi nane).
Wakati ngome ya vijana nafasi zinazogombewa ni mwenyekiti, makamu mwenyekiti Bara na Zanzibar, katibu na naibu wake, wajumbe wa halmashauri kuu Taifa na wajumbe wa mkutano mkuu.
Miongoni mwa waliochukua fomu kugombea nafasi mbalimbali katika chama hicho ni pamoja na Maalim Seif na Yeremia Maganja (uenyekiti), Zitto Kabwe na Ismail Jussa (kiongozi wa chama), Juma Duni Haji (makamu mwenyekiti Zanzibar), Dorothy Semu na Riziki Ngwali (makamu mwenyekiti bara).