Dodoma. Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nnauye amehoji sababu za Serikali ya Tanzania kutenga fedha kidogo za maendeleo katika bajeti ya Wizara ya Kilimo wakati ikijulikana kuwa asilimia 70 ya Wanzania ni wakulima.
Nape ametoa kauli hiyo leo Jumanne Juni 18, 2019 bungeni jijini Dodoma katika mjadala wa Bajeti ya Serikali mwaka 2019/2020 ya Sh33.1 trilioni.
Bajeti ya Wizara ya Kilimo mwaka 2019/2020 ni Sh253.85 bilioni zikiwemo Sh143.57 bilioni za maendeleo.
“Bajeti yetu kwa sehemu kubwa fedha nyingi zimepelekwa kwenye maeneo ya ujenzi na miradi mikubwa tuliyonayo (reli ya kisasa (SGR), mradi wa umeme na ununuzi wa ndege), si jambo baya lakini sekta inayohusisha watu wengi ni kilimo.”
“Kilimo kinazalisha ajira asilimia 65 na asilimia 85 ya bidhaa tunazouza nje zinatokana na kilimo. Kilimo kinachangia pato la taifa kwa asilimia 29 na asilimia zaidi ya 100 chakula nchini kinategemea kilimo,” amesema Nape.
Amesema kilimo ni sekta inayotakiwa kuguswa kikamilifu ili kupambana na umasikini wa watu.
Pia Soma
- Watumishi wa TRA Geita wadakwa wakiomba rushwa ya Sh100 milioni
- Polisi Geita yawadaka watatu wakijifanya maofisa usalama
- LIVE: MWILI WA MWANAFUNZI WA CHUO KIKUU KAMPALA UKIAGWA
“Hili ndilo eneo kubwa na kupanga ni kuchagua. Kama tunataka kushughulika na umasikini na watu wengi zaidi fedha nyingi zingekwenda huko,” amesema Nape.
Amesema kama fedha hazipelekwi kama inavyotakiwa unatakiwa kurudishwa utaratibu wa mwaka 2016/17 wa kufuta tozo mbalimbali katika sekta ya kilimo.
“Katika mapendekezo ya Serikali katika bajeti ya 2019/2020 tumejikita kwenye tozo katika baishara ila kwenye kilimo tumefumba macho,” amesema Nape.