Dar es Salaam. Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa amesema ana uhusiano na Rais wa Tanzania, John Magufuli na kutaka mambo ya familia pamoja na kiongozi mkuu huyo wa nchi yaachwe yazungumzwe kifamilia na si kujadiliwa na CCM wala Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa.
Msigwa ameeleza hayo leo Ijumaa Machi 13, 2020 katika mkutano na waandishi wa habari ofisi za makao makuu wa Chadema mtaa wa Ufipa Dar es Salaam, ikiwa imepita siku moja tangu Rais Magufuli kumlipia faini ya Sh38 milioni.
Ametoa kauli hiyo wakati akizungumzia tukio la kiongozi mkuu huyo wa nchi kumlipia faini, huku Chadema nao wafanya hivyo kitendo ambacho kimezungumzwa kwa nyakati tofauti na Gerson Msigwa na katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Humphrey Polepole.
Katika maelezo yake Mchungaji Msigwa amesema, “mimi na Magufuli tuna uhusiano, Polepole na Msigwa (Gerson) sio wasemaji wa familia hivyo mambo ya kifamilia tunayazungumza kifamilia. Jana nikiwa gerezani niliitwa nikatoka nje nikakuta kuna kamera nataka kurekodiwa nikarudi ndani (gerezani) na kuwakacha.”
“Mimi ni mtu ninayejitambua siwezi kununuliwa kwa pesa mimi na Magufuli tuna uhusiano hata chama changu kinajua.”
Viongozi walioachiwa hadi sasa ni Katibu Mkuu, John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu, Salum Mwalimu na mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche na Mbunge wa Iriinga Mjini Peter Msigwa.
Habari zinazohusiana na hii
- Kauli ya CCM kuhusu Magufuli kumlipia faini mchungaji Msigwa
- Mbowe alipa faini, muda wowote kutoka jela
- VIDEO: Mzozo waibuka wakati Heche, Mnyika, Salum Mwalimu wakitoka Segerea
- VIDEO: Mnyika, Heche na Mwalimu watoka jela
Taarifa iliyotolewa na naibu katibu mkuu (Bara), Benson Kigaila inaeleza kuwa Mbowe ameshalipiwa faini ya Sh70 milioni na wakati wowote atatoka jela.
Amesema chama hicho kimekusanya Sh312 milioni kuanzia Jumanne jioni, zimetumika kuwalipia faini viongozi.