Unguja. Kukutana kwa vyama 15 ya upinzani visiwani Zanzibar leo Jumanne Desemba 18, 2018 inaelezwa kuwa huenda ikaibuka historia mpya ya ushirikiano baada ya Ukawa kuonekana kutetereka tangu kumalizika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Vyama hivyo vinakutana kwenye mkutano wa faragha ulioratibiwa na Chama cha Wananchi (CUF) uliokuwa na ajenda kuu tatu, ikiwamo ya udhaifu wa Ukawa inayoundwa na vyama vinne vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Mbali na ajenda ya Ukawa, pia vinajadili namna watakavyoshiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2019 na Uchaguzi Mkuu wa 2020 na namna ya kufanya siasa katika kipindi hiki ambacho demokrasia inaminywa.
Ajenda nyingine ni namna ya kukisaidia CUF kilichokumbwa na mgogoro wa uongozi wa muda mrefu uliokipasua vipande viwili.
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe na Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad ni miongoni mwa washiriki wa mkutano huo.
Desemba 9, 2018 vyama hivyo 15 vilitoa tamko la pamoja jijini Dar es Salaam kupinga muswada wa marekebisho ya sheria ya vyama vya siasa kwa maelezo kuwa una vipengele vingi vinavyovikandamiza vyama hivyo na kuwataka wabunge na wadau wa siasa kuupinga.