Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ufanisi, upekee Uchaguzi Mdogo Jimbo la Ngorongoro

5dc065f780043e2677e099e11658f95a.png Ufanisi, upekee Uchaguzi Mdogo Jimbo la Ngorongoro

Wed, 29 Dec 2021 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Desemba 11, mwaka huu (2021) wananchi wa Jimbo la Ngorongoro walipiga kura kwenye uchaguzi mdogo wa jimbo hilo kujaza nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo na Naibu Waziri, Ofisi ya

Waziri Mkuu, Uwekezaji, William Tate Ole Nasha.

Uchaguzi huo umefanyika baada ya Spika wa Bunge la Tanzania kutekeleza matakwa ya kifungu namba 37 (3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi.

Kifungu hicho kinasema: “Endapo mbunge anajiuzulu, kufariki au anaachia ofisi yake kwa sababu nyingine tofauti na zile zilizopo chini

ya kifungu cha 133 (kuhusu kesi inayosubiria uamuzi wa mahakama), Spika kwa maandishi kwa Mwenyekiti wa Tume na kwa taarifa itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali, atatangaza kwamba kuna nafasi katika kiti cha ubunge.”

Halmashauri ya Wilaya Ngorongoro lilipo Jimbo la Ngorongoro ni mojawapo kati ya halmashauri za wila-

ya sita na jiji moja zilizopo katika Mkoa wa Arusha.

Makao makuu ya wilaya yapo Loliondo Wasso umbali wa takribani kilometa 400 kutoka makao makuu ya mkoa. Wilaya hii ilianzishwa mwaka 1979 chini ya Sheria Namba 5 ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 ikiwa na tarafa tatu za Loliondo, Sale na Ngorongoro. Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCA) imo ndani ya Wilaya ya Ngorongoro.

Wilaya hii imegawanyika kwenye maeneo makuu matatu ambapo eneo lililopo chini ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro lina ukubwa wa kilometa za mraba 8,292 sawa na asilimia 59 za eneo lote la wilaya. Eneo hili la hifadhi hutumika kwa malisho ya mifugo na wanyamapori na pia shughuli za kitalii.

Eneo la pili ni pori tengefu la Loliondo linalojumuisha tarafa yote ya Loliondo na sehemu ya Tarafa ya Sale lenye ukubwa wa kilometa za mraba 4,000 sawa na asilimia 28.4. Eneo hili hutumika kwa shughuli za kilimo, ufugaji, hifadhi ya wanyama, misitu, biashara, utalii na makazi.

La tatu ni eneo la pori tengefu la Ziwa Natron linalojumuisha sehemu iliyobaki ya Tarafa ya Sale lenye ukubwa wa kilometa za mraba 1,744 sawa na asilimia 12.4.

Kwa jiografia hiyo ya Jimbo la Ngorongoro na kwa kuzingatia ukweli kwamba eneo kubwa lipo kwenye hifadhi ambayo pia wananchi wanaishi, uchaguzi wa jimbo hili ulikuwa wa kipekee kutokana na jinsi wakazi wa jimbo walivyosambaa na changamoto ya miundombinu duni hasa ya barabara kufika kwenye maeneo wanakoishi wapiga kura.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa mujibu wa Ibara ya 74 (6) ya Katiba ya nchi, imepewa jukumu la kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi wa wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na madiwani kwa Tanzania

Bara. Hii ni pamoja na chaguzi ndogo zinazojitokeza kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo vifo, kujiuzulu au kufukuzwa chama.

Kama ilivyo ada baada ya kifo cha Ole Nasha, Tume ilipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye kwa kuzingatia kifungu cha 37(3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, aliitaarifu Tume uwepo wa nafasi wazi ya Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro katika Halmashauri ya Ngorongoro mkoani Arusha.

Mwenyekiti wa Tume, Jaji Semistocles Kaijage akautangazia umma ratiba ya uchaguzi huo mdogo.

Kwa mujibu wa ratiba iliyokuwa imepangwa na Tume wagombea walichukua fomu kuanzia Novemba 9 hadi 15, 2021 na siku ya uteuzi ilikuwa Novemba 15, mwaka huu. Kampeni za uchaguzi zilifanyika kuanzia Novemba 16 hadi Desemba 10 na siku ya uchaguzi ilikuwa Desemba 11, mwaka huu.

Ikumbukwe kwamba katika ngazi ya uteuzi wa wagombea NEC kwenye tarehe iliyopangwa ilifanya uteuzi wa wagombea 11 ambao walipendekezwa na vyama vyao. Wagombea hao waliteuliwa baada ya kutekeleza masharti ya uteuzi kabla ya saa 10 kamili jioni siku ya uteuzi.

Miongoni mwa masharti ambayo msimamizi wa uchaguzi wa jimbo ana wajibu wa kuyazingatia kabla ya uteuzi wa mgombea wa nafasi ya ubunge ni pamoja na kujiridhisha kuwa Fomu ya Uteuzi Na. 8B na Fomu Na. 10 ya kuheshimu na kuzingatia maadili ya uchaguzi zimejazwa kikamilifu.

Kwa uchaguzi wa Jimbo la Ngorongoro, wagombea 11 waliotimiza masharti na vigezo vya kuteuliwa na majina ya vyama vyao kwenye mabano ni Zuberi Hamisi (ADA TADEA), Bayo Johnson (SAU), Amina Mcheka (NLD) na Mary Daudi (UPDP).

Wengine ni Shangai Lekishon (CCM), Feruziy Feruziyson (NRA), Simon Ngilisho (Demokrasia Makini), Johnson Gagu (ACTWazalendo), Shafii Kitundu (ADC), Frida Nnko (UMD) na Paulo Makuru (UDP).

Wagombea hao walipata fursa ya kufanya kampeni kwa mujibu wa ratiba zilizowasilishwa na vyama vyao kwa msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo ambapo wapiga kura walipata fursa ya kushiriki na kusikiliza sera na ahadi mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na wagombea hao.

Tume katika kipindi hicho cha uchaguzi licha ya mazingira magumu ya jimbo hilo, ilifanya maandalizi yote ya uchaguzi huo kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya mpiga kura ambalo

ni jukumu la Tume kwa mujibu wa kifungu cha 4C cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343. Kifungu hicho kinaipa Tume jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura kwa nchi nzima, kuratibu na kusimamia watu wanaotoa elimu hiyo.

Kwa kutumia gari maalumu la matangazo, Tume ilitembelea takribani kata zote za Jimbo la Ngorongoro na kutoa elimu ya mpiga kura kwa wananchi wa maeneo hayo ikiwa ni pamoja na kusambaza vipeperushi na kujibu maswali mbalimbali ya wananchi.

Kutokana na changamoto ya miundombinu mibovu ya barabara timu ya gari la matangazo ilifanikiwa kufika kwenye kata 20 kati ya kata 28 za jimbo hilo.

Hata hivyo, elimu ya ana kwa ana na nyumba kwa nyumba iliyotolewa baada ya elimu kwa njia ya gari la matangazo, ilifika kwenye kata zote 28.

Pia katika utoaji wa elimu ya mpiga kura ilionekana kwamba wapiga kura wengi waliopoteza kadi za kupigia kura hawakuwa na vitambulisho mbadala ambavyo Tume iliruhusu vitumike kupigia kura kwa waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, vitambulisho hivyo ni pamoja na pasi ya kusafiria, leseni ya udereva na kitambulisho cha taifa kilichotolewa na NIDA.

Hata hivyo, Tume ilifanikiwa kusambaza vifaa vya kupigia kura kwa wakati na siku ya uchaguzi vituo vilifunguliwa saa moja kamili asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na matokeo ya uchaguzi huo yalitangazwa saa tano asubuhi siku iliyofuatia Desemba, 12.

Kuchelewa huko kunatokana na ugumu uliokuwepo wa kusafirisha vifaa kutoka kwenye vituo vya kupigia kura hadi kwenye kituo kikuu cha kujumuishia matokeo kilichokuwepo kwenye makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro.

Ikumbukwe kwamba kwenye chaguzi zilizopita ilikuwa inachukua mpaka siku mbili kwa matokeo ya jimbo hilo kutangazwa hivyo katika uchaguzi huu jitihada kubwa zilifanyika.

Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Msimamizi wa Uchaguzi, Dk Juma Mhina katika uchaguzi huo mgombea kwa tiketi ya CCM, Shangai Lekishon aliibuka mshindi wa uchaguzi huo baada ya kupata kura 62,017 kati ya kura 62,461 halali zilizopigwa.

Jumla ya wapiga kura 62,528 walipiga kura kati ya wapiga kura 115,838 walioandikishwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

Mwandishi wa Makala haya ni Ofisa Habari Mwandamizi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live