Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ubinafsi kilio kwa Afrika

Ef39e13a39b45366d621a587631a9cb1.png Ubinafsi kilio kwa Afrika

Wed, 22 Dec 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

KWA wafuatiliaji wazuri wa masuala ya kisiasa watakumbuka kwa kina kilichotokea siku ambayo Edward Moringe Sokoine, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania alipotembelea Kibaha mkoani Pwani kutimiza majukumu ya kuwatumikia wananchi na kukaribishwa chakula katika moja ya shule za msingi.

Kabla watu hawajaanza kufaidi msosi huo, Sokoine akauliza: “Hivi hawa watoto (yaani wanafunzi) waliopo hapo nje wamenisubiri tangu saa ngapi? Akajibiwa kuwa tangu asubuhi ya siku hiyo.

Akauliza: “Wameshakula?” Hakupata jibu.

Akasema: “Mimi ninarejea Dar es Salaam na hivyo kila mtu akale kwake. Hiki chakula wapeni hawa watoto wale.”

Kwa waliokuwepo hasa maofisa wakubwa inasemekana walichukia sana. Kuchukia kwao kulikuwa na mengi kwamba walikuwa na njaa wakakaribia meza kisha wakatolewa kapa!

Kisa hiki kinafanana na kile nilichowahi kusikia kwamba Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alifika mkoa fulani Tanzania hii akiwa ziarani alipoalikwa chakula akauliza kama dereva wake ameshakula akajibiwa hapana.

Waliokuwepo wanaeleza kwamba, Nyerere alimuita dereva wake akala kisha aliposhiba wakaondoka hakula chakula hicho hata kidogo.

Ndugu msomaji, leo nimeanza kwa kuonesha visa vya viongozi hao wa Tanzania ambao sasa hawapo tena duniani na jinsi walivyotanguliza maslahi ya wanaowaongoza kuliko yao ili kuleta maana halisia katika makala haya.

Kimsingi wanamajumuhi watakubaliana na mimi kwamba mawazo ya wazee wetu wapigania Uhuru Afrika walikuwa wazalendo sana. Walitanguliza maslahi ya walio wengi yaani wananchi wao kuliko wao wenyewe.

Kwa nyakati tofauti imesikika mataifa makubwa yakiwataja viongozi wa Afrika kuwekeza fedha zao nyingi katika nchi za wenzetu huko ughaibuni; wakati huo huo wakiwakamata watakatisha fedha katika nchi husika.

Sasa najiuliza wakati wanawakamata watakatisha fedha leo, nafsi zao huwa haziwasuti? Kinachoniuma

zaidi viongozi na wasomi waliosogea kiumri kwenye nchi zetu hizi wamesomeshwa na nchi zao.

Lakini je, wanazitendea haki nchi zao? Wanatendea haki kodi za walala hoi? Wanakumbuka bila kujitoa kwa Waafrika, wapigaji hao pengine wasingepata kuwa kama walivyo sasa?

Ukweli dhana ya ubinafsi baina ya viongozi walio wengi katika Bara la Afrika ni kubwa sana. Viongozi hawa wa kisiasa wamekuwa wakitanguliza maslahi yao pasipo kuona haya hata kidogo. Ni rahisi kuingiza nchi katika mikataba mibovu kwa lengo tu apate asilimia 10.

Miradi inaanzishwa

mikubwa lakini ndani yake kuna kuvutia upande wao na pengine hata kuhakikisha inawanufaisha wao wenyewe. Huruma kwa wananchi imepungua kabisa. Kinachoangaliwa ni umimi.

Hata kwenye uchukuaji wa mikopo ya Covid-19 wadadisi wa mambo wanaonesha kwamba fedha hizo za mikopo zimewanufaisha viongozi kuliko wananchi walio lengwa. Ni kosa mbele za Mungu na watu wake kufanya mambo yanayoumiza watu kwa ubinafsi wa namna hii.

Umimi umesababisha Bara la Afrika lisiungane. Kila mmoja ana uchu wa madaraka. Kila mmoja ana-

taka kuonekana ana nguvu kubwa ya kupigiwa ving’ora kila anapopita. Kwasababu ya umimi bara limeendelea kutawaliwa na ukoloni mamboleo.

Kwa sasa Waafrika wananyanyasika kila kona ya dunia kwa sababu ya uzembe wa ubinafsi wa wachache. Mawazo ya wapigania uhuru ukiachilia mbali Nelson Mandela wa Afrika Kusini yalikuwa ni kuifanya Afrika taifa moja lenye kiongozi mmoja na viongozi wa majimbo ambayo ndio nchi.

Iwapo hili lingefanyika basi leo hii hakuna taifa tajiri na lenye nguvu lingekuwa linaizidi Afrika. Bahati mbaya wazee hawa ndoto

zao ziliambatana na vifo vyao. Leo hii, Afrika ina utabaka wa kinchi na kifikra. Uchu wa madaraka umetawala.

Kwame Nkrumah (hayati) akihutubia Taifa la Ghana enzi za uhai wake alisema: “Ipende Ghana kwa moyo wako wote, kiasi kwamba unaweza kujitoa mhanga kwa ajili ya taifa lako bila kusita.”

Maneno haya aliyatoa kuwakumbusha wananchi wa Ghana juu ya umuhimu wa kupenda taifa lao pasipo kusita wala kujiuliza swali lolote. Kutanguliza maslahi ya wana Ghana wote. Leo hii je, hali ikoje?

Dhana ya umimi katika uchu wa madaraka inayowatesa wanasiasa wa kileo haikuwa hivyo enzi za wapigania uhuru yaani wana majumuhi.

Nkrumah pia aliwahi kusema: “Niko tayari kufanya kazi katika Afrika iliyoungana na kuongozwa na kiongozi yeyote ambaye yuko tayari kuongoza taifa la Afrika kwa uangalizi mzuri na maelekezo timamu.”

Wakati Nkrumah akisema haya, Mwalimu Nyerere kwa kinywa chake alisema wakati akipigania Uhuru wa Tanganyika kuwa ni matamanio yake kuwa na Taifa la Afrika Mashariki.

Nyerere alikuwa tayari kufanya kazi chini ya Jomo Kenyata (marehemu) na kwamba aliamini ndiye alifaa kuwa Rais wa Afrika Mashariki kama ingeungana. Maono haya ya kutojitanguliza wao viongozi hawa wa Afrika yamepotelea wapi?

Leo hii haramu, tunaifanya

halali eti tu kuwafurahisha wakubwa. Tuko tayari kujidhalilisha kama Waafrika kwa lengo tu la kupata fedha kutoka kwa wale waliotutawala huku ajenda zao wengi (si wote) zikiwa na siri ndani yake.

Ubinafsi huu unasababisha watu kuanzisha vyama vyao binafsi vya kisiasa ili tu kinachopatikana kiwanufaishe wao. Wafanyabiashara wakubwa wanajificha nyuma ya vyama vya kisiasa kwa kudhamini shughuli za vyama ili baada ya dhamana hiyo wapewe misamaha ya kodi.

Kama ilivyo kawaida

vyama hivi vinashiriki chaguzi lakini kiuhalisia vyama hivi vingi ni mali za watu binafsi, havijabeba dhamana ya wananchi kama zisemavyo katiba zao.

Ni ubinafsi huu huu unaosababisha maliasili zisiwanufaishe wananchi wengi badala yake watu wachache ambao wanakula na wakubwa (yaani viongozi wa kisiasa) Afrika. Kukitokea mtu wa kukemea basi anatengenezewa mazingira ya kuonekana hafai kwenye jamii.

Ndugu msomaji, dhana ya ubinafsi katika Bara la Afrika haishii kwa wanasiasa

tu bali hata kwa mtu mmoja mmoja. Hata hivyo, ni jambo linaloepukika iwapo kutakuwepo utashi wa kisiasa na utu. Tukishinda hili hakutakuwepo ulimbikizwaji wa mali nyingi za wizi kwa mtu mmoja ambaye pengine ni kiongozi wa kisiasa.

Neema ya Mungu, bidii ya kazi, uwazi, utu wema ndiyo itakayolisaidia Bara la Afrika kama kweli tunataka kuondokana na ukoloni mamboleo.

Mwandishi ni mchangiaji wa makala wa gazeti hili, mawasiliano yake ni +255712246001; [email protected]

Chanzo: www.habarileo.co.tz