KATIBU Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wa CCM, Queen Mlozi amesema jumuiya hiyo itawapigania wagombea wanawake ili kushinda katika nafasi walizojitosa za kuwania ubunge, udiwani na uwakilishi katika uchaguzi ujao.
Mlozi alitoa kauli hiyo wakati akitoa tamko la kuwahamasisha wanawake nchini kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ukiwemo ubunge, udiwani na uwakilishi.
Alisema UWT imejipanga kuhakikisha inawatendea haki wanawake bila upendeleo na kuwataka waendelee kuchukua fomu za kugombea nafasi hiyo ili kupata uongozi.
“Wanawake wenye vigezo kutoka makabila yote na dini zote, wachukue fomu za kugombea uongozi ili tuweze kupata wawakilishi wengi bila kujali au kuogopa chochote na UWT haitamuacha mwanamke aliyethubutu kwa sababu uwezo tunao,
“Ninaomba niwahakikishie kuwa jumuiya imejipanga vizuri kuhakikisha inawatendea haki wanawake wote bila kujali ubaguzi wowote, hivyo wanawake mnayo fursa za kugombea.”
Kuhusu mchakato wa kupata wawakilishi, katibu mkuu huyo alisema wamejipanga kuanzia kwenye ngazi ya kata, wilaya, mkoa na taifa ili kuhakikisha haki inatumika pasipo upendeleo wowote.
Alisema uchaguzi wa mwaka huu, utakuwa tofauti na miaka mingine kwani utakuwa wa wazi na kila kitu kitafanyika hadharani hakutakuwa na ujanja ujanja wala udanganyifu.
“Kwa wale watakaopita kwenye mchakato mbalimbali wa uchaguzi tunawahakikishia hakutakuwa na upendeleo wa aina yoyote, na tumejipanga vizuri kuanzia ngazi ya chini hadi juu ili kuhakikisha haki inatumika, ilitupate watu wenye sifa ambao watakuwa viongozi bora.
“Vivyo hivyo, uteuzi utakaofanyika baada ya uchukuaji wa fomu, utakuwa uteuzi uliozingatia kanuni za uteuzi za wagombea katika vyombo vya dora uliotolewa na CCM,” alisema.