Dodoma. Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) limefanya uchaguzi wa wajumbe wanne wa kamati ya utendaji ya baraza hilo na kuwathibitisha wakuu wa idara tano za umoja huo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi Septemba Mosi, 2018 katibu mkuu wa UVCCM, Raymond Mwangwala amesema kati ya waliochaguliwa wawili wanatoka Tanzania bara na wawili Zanzibar.
“Kwa upande wa Tanzania bara tumemchagua Saitoti Steven na Joanfaith Kataraiya na kule Zanzibar tumemchagua Abdulghafar Idrissa Juma na Mariam Ally Juma,” amesema Mwangwala.
Amesema walipokea na kuwathibitisha wakuu wa idara tano za umoja huo ambao ni Peter Kasera ambaye amekuwa katibu wa idara ya organaizesheni, siasa na ushusiano wa kimataifa.
Amesema wengine ni Lusekelo Nelson ambaye ni katibu wa idara ya uchumi, uwekezaji na fedha; Kamana Simba, katibu wa idara ya vyuo na vyuo vikuu; Hassan Bomboko katibu wa idara ya uhamasishaji na chipukizi pamoja na Mohammed Abdalla ambaye ni katibu wa idara ya usalama na maadili.