Dar es Salaam. Ikiwa kesho ndiyo siku ya mwisho ya uandikishaji wa Daftari la Wapiga kura kama ilivyoelezwa awali, Serikali imeongeza siku tatu za mchakato huo ili kuwapa fursa Watanzania wengi kujiandikisha.
Leo Jumapili, Oktoba 13, 2019 katika mtandao wa kijamii wa Facebook wenye akaunti ya Ofisi ya Rais (Tamisemi), imewekwa taarifa inayoeleza kuwa Waziri wa ofisi hiyo, Seleman Jafo ameongeza siku hizo na sasa mchakato huo utamalizika Oktoba 17, 2019.
Kabla ya kutangazwa taarifa hiyo, Oktoba 11, akiwa mkoani Katavi kwenye ziara ya kikazi ya Rais wa Tanzania, John Magufuli, Waziri huyo aliahidi kupeleka mapendekezo maalumu kwa Rais kuomba mikoa itakayofanya vibaya iongezewe muda wa uandikishaji.
Alikuwa akitoa taarifa ya hali ya uandikishaji kwenye mikoa mbalimbali wa Daftari la Wapiga kura.
Lakini jana Oktoba 12, Rais Magufuli. akizungumza wakati wa uzinduzi wa safari za Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) mkoani Katavi, alisema mikoa ambayo viongozi wake watashindwa kuwahamasisha wananchi kujiandikisha ili wapige kura atawashangaa huku akisema hadhani kama atalaumiwa na Watanzania kwa hatua atakazozichukua.
“Waziri (Jafo) ametoa takwimu za baadhi ya mikoa iliyofanya vizuri. Ninafuatilia lakini alitoa iliyofanya vibaya, mchakato ukikamilika nitataka anipe taarifa ya mikoa iliyofanya vizuri na vibaya,” alisema Rais Magufuli kwenye ziara hiyo.
Pia Soma
- Makonda aagiza maduka yote Dar kesho yafunguliwe saa 5 asubuhi
- Tanzania yashauriwa kutumia teknolojia ya datawazi
- LHRC waibua hoja ya Katiba mpya