Dar es Salaam. Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye ameitaka Tume ya Uchaguzi (NEC) kutenda haki katika uchaguzi mdogo utakaofanyika Septemba 16, 2018 ili kuepuka machafuko.
Sumaye ambaye ni mwenyekiti wa Chadema kanda ya Pwani na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi jimbo la Ukonga ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Septemba Mosi, 2018 katika mkutano na waandishi wa habari.
Amesema tume hiyo haipaswi kupendelea upande wowote wa chama cha siasa, badala yake ihakikishe uchaguzi unafanyika bila kuonewa mtu.
"Tumeshuhudia chaguzi nyingi zinaingia dosari ikiwemo mawakala kucheleweshewa barua zao huku wengine wakilalamikia kutangazwa mgombea ambaye hajashinda,” amesema.
Ameitaka NEC kuwa huru na kutokubali kuingiliwa na mhimili mwingine katika utendaji wake wa kazi kwenye uchaguzi huo.
"Tunataka tume iwe huru isiogope kufanya kazi yao kwa ufasaha kwa sababu ya vitisho, sisi tunawahakikishia wananchi kuwa watadumisha amani na tutapokea matokeo kwa moyo mkunjufu ili mradi yawe ya haki,” amesema.