Mbeya. Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu Sugu amesema wagombea udiwani wa chama hicho wataibuka na ushindi katika uchaguzi mdogo utakaofanyika kesho katika kata tatu mkoani humo.
Sugu ametoa kauli hiyo leo katika mkutano wa mwisho wa kampeni uliofanyika viwanja vya mtaa wa Ilembo kata ya Lwabi jijini hapa.
“Ndugu zangu kesho lazima tutoboe kata zote maana tukiacha hawa jamaa watajidai sana. Lazima tuwaonyeshe kuwa hii ndiyo Mbeya.”
“Tunajua mbinu zao zilizobaki ni polisi tu lakini wanajua wazi hawana chao na sasa wanaweweseka,” alisema.
Alidai baadhi ya viongozi wamekuwa wakiwatisha watu kuelekea uchaguzi huo na kuwataka wananchi kutokuwa na hofu yoyote kwani kupiga kura ni haki yao.
“Napenda kuwaeleza polisi na NEC (Tume ya Taifa ya Uchaguzi) wawaache wananchi wakapige kura, mkijaribu kuvuruga uchaguzi huu na nyuso hizi za wananchi mnaziona hatutakubali kuonewa,” alisema.