Spika wa Bunge la Tanzania, Dk Tulia Akson amemuapisha Tamima Haji Abass kuwa mbunge wa Bunge la Muungano leo Jumanne Septemba 13, 2022.
Tamima amekula kiapo hicho akichukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa mbunge wa Viti Maalum, Irene Ndyamkama ambaye alifariki dunia April 24,2022.
Kwa kuwa Marehemu Irene alikuwa Mwakilishi aliyetokea CCM, mwongozo unataka Tume ya Taifa ya Uchaguzi kupeleka jina la mtu anayeziba nafasi akiwa ametoka chama hicho isipokuwa Marehemu kama angekuwa mbunge wa kuchaguliwa kwa Jimbo ambapo vyama vingeshindanishwa.
Tofauti na ilivyo wakati wa viapo vingine, leo wakati wa kiapo cha mbunge huyo hakukuwa na shamrashamra kubwa kama ilivyozoeleka.
Kwa wabunge wa Viti Maalum, Ndyamkama alikuwa mbunge wa pili kupoteza maisha baada ya aliyekuwa mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Manyara, Martha Umbura lakini hadi sasa Bunge la 12 limeshapoteza wabunge sita.