Spika wa Bunge Job Ndugai amesema kuwa ofisi ya Bunge itagharamia viburudisho kwa wabunge tu wawapo katika vyumba vya watu maarufu (VIP) kwenye viwanja vya ndege.
Ndugai ametoa ufafanuzi huo leo Ijumaa Septemba 10 2021 mara baada ya kipindi cha maswali na majibu.
Amesema wabunge wanayo haki ya kutumia ukumbi wa watu maarufu (VIP) kwenye viwanja vya ndege vyote nchini.
Hata hivyo, amesema huduma za viburudisho ni kwa wabunge tu na sio kwa wenza wao wala wasindikizaji wawapo katika vyumba hivyo.
“Ofisi ya Bunge inawajibika kugharamia gharama za viburudisho tu kwa wabunge sio unaenda pale unaagiza Lager kubwa Castle (aina ya bia),”amesema.
Amesema pale ambapo mbunge anandamana na mwenza wake ama msindikizaji inambidi amlipie yeye mwenyewe.
“Nadhani tumeelewana naomba mzingatie hayo,”amesema Spika Ndugai.