Dodoma. Wabunge wa vyama vya upinzani leo Alhamisi Juni 13, 2019 bungeni jijini Dodoma wamesimama kwa takribani dakika tatu huku wakizomea na kupiga meza baada ya kuelezwa kuwa moja ya sifa ya wagombea katika uchaguzi wa Serikali za mitaa ni kuwa wanachama wa CCM.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango wakati akiwasilisha bajeti ya Serikali mwaka 2019/2020 ambayo ni Sh33.1 trilioni.
Wakati akihitimisha kuwasilisha kusoma bajeti hiyo, Dk Mpango aligusia uchaguzi huo utakaofanyika Oktoba 2019 kuwa ni kuchagua mtu anayetoka CCM.
"Sifa ya 10 awe anatoka ndani ya chama cha siasa kinachotetea maslahi na haki za wanyonge na chama hicho ni CCM, " amesema Dk Mpango.
Baada ya kauli hiyo ambayo Dk Mpango aliirudia mara tatu, wabunge wa upinzani walisimama huku wakipiga meza zao na kuimba "CCM, CCM, CCM. "
Wakati wapinzani wakiwa wamesimama, wabunge wenzao wa CCM nao walisimama na kusababisha Dk Mpango kusimama kuwasilisha bajeti hiyo kwa dakika tatu.
Pia Soma
- Spika Ndugai asema Bajeti imelenga kuondoa utitiri wa kodi
- Uzalishaji wa dhahabu wapungua Tanzania
- Soma hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango akiwasilisha bungeni mapendekezoya Serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2019/20
- Serikali yafuta tozo ya kushikilia dawa za chanjo na mitishamba
Dk Mpango alipopewa nafasi ya kuendelea kuwasilisha amesema alichokisema kina baraka ya Rais John Magufuli.