Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Shinyanga yapata hati safi, mkuu wa mkoa ajivunia

BARAZA L Shinyanga yapata hati safi, mkuu wa mkoa ajivunia

Sat, 25 Jun 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga imepata hati safi katika majibu ya ukaguzi yaliyotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika mwaka wa fedha 2020/2021, huku Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema akiagiza waliosababisha hoja za CAG na kukimbia wasakwe.

Manispaa ya Shinyanga ilikuwa na hoja 79, ambazo zilikuwa zimeibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambapo kati ya hoja hizo imejibu 38.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Jomaary Satura, amebainisha hayo leo Juni 25,2022, kwenye kikao maalum cha Baraza la Madiwani cha kujadili taarifa ya CAG.

Amesema Manispaa ya Shinyanga katika majibu yaliyotolewa na CAG, baada ya kujibu hoja 38 zilizoibuliwa katika mwaka huo wa fedha (2020/2021) unaoishia Juni 30 imefanikiwa kupata hati safi.

"Majibu ya utekelezaji wa hoja za ukaguzi kama zilivyotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG),kwa kipindi kinachoishia juni 30, 2021 Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga tumepata hati safi," amesema Satura.

"Manispaa ya Shinyanga ilikuwa na hoja 79, hoja ambazo zimejibiwa na kufungwa ni 38, na hoja 41 zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji," ameongeza.

Naye Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amewataka watendaji wawe waadilifu katika utekelezaji wa majukumu yao, kutunza nyaraka za miradi wakati wa manunuzi, pamoja na kupeleka pesa benki za makusanyo ya mapato ili kupunguza hoja.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, amewataka watendaji wa Halmashauri wawe wanajibu vizuri hoja za CAG ili kupunguza wingi wa hoja, sababu baadhi ya hoja zinatokana kwa kutojibiwa vizuri.

"Tunataka halmashauri zetu ziendelee kupata hati safi, lakini hoja ziwe chache na kufutika," amesema Mjema.

Katika hatua nyingine, ameagiza baadhi ya watu na watumishi wa Serikali, ambao walifanya ubadhilifu wa fedha kwenye miradi na kukimbia, wasakwe popote walipo ili wachukuliwe hatua, na kufuta hoja za CAG juu ya miradi hiyo.

Kwa upande wao baadhi ya madiwani, wamesema baadhi ya hoja ambazo zimekuwa zilijirudia mara kwa mara zifanyiwe kazi na kufutwa.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live