Dar es Salaam. Shahidi wa saba katika kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania Chadema, akiwemo Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kuwa wabunge wote huwa hawachaguliwi kuwa mawakala wa kusimamia uchaguzi.
Shahidi huyo Victoria Wihenge (34) ambaye ni Ofisa Uchaguzi Manispaa ya Kinondoni, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, leo Alhamisi Agosti 29, 2019 wakati akihojiwa na mawakili wa upande wa utetezi.
Wihenge ametoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba.
Shahidi huyo amedai kwa mujibu wa sheria na taratibu za uchaguzi, wabunge huwa hawana sifa za kuwa mawakala kwa sababu wote wanakuwa ni waheshimiwa.
Wihenge ameeleza hayo wakati alipoulizwa swali na Wakili wa utetezi, John Mallya aliyetaka kujua iwapo washtakiwa tisa ambao ni viongozi wa Chadema waliopo mahakamani hapo kama walikuwa mawakala katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Kinondoni, Dar es Salaam.
Upande wa utetezi kutumia video kumhoji shahidi kesi ya kina Mbowe
Pia Soma
- Ethiopia wagundua fuvu la binadamu lenye miaka milioni 3.8
- Polisi Dar yasema waliokamatwa wakiandamana kushinikiza ndege ya ATCL kuachiwa watachukuliwa hatua
- Lugola asema Tanzania ni nchi salama kwa wananchi na mali zao
- Wakulima Tanzania watahadharishwa, watakiwa kuweka akiba ya chakula
Wakili Mallya: Nikisema washtakiwa hawa waliopo mahakamani hapa wote walikuwa ni mawakala katika uchaguzi uliofanyika Februari 17, 2018 utabisha?
Shahidi: Ndio
Mallya: Nini kinachofanya ubishe?
Shahidi: Hawakuwa mawakala
Mallya: Nini kinachofanya wasiwe mawakala?
Shahidi: Hawana sifa kwa sababu wote ni waheshimiwa.
Shahidi: Ili uwe wakala lazima ule kiapo, sasa hao wote hawakula kiapo kwa ajili ya kusimamia uchaguzi.
Mallya: Hata Salum Mwalimu naye hakula kiapo?
Shahidi: Mgombe wa ubunge kwa tiketi ya Chadema, Mwalimu( anamtaja kwa jina moja) hakuwa katika orodha ya mawakala 613 waliokula kiapo.
Mallya: Halima Mdee ni Mbunge wa wapi?
Shahidi: Mbunge wa Kawe.
Mallya: Dk Mashinji ni Mbunge wa wapi?
Shahidi: Sifahamu.
Mallya :Lakini ni Mbunge?
Shahidi: Sikumbuki
Mallya: Umesema wabunge hawana sifa za kuwa mawakala kwa sababu ni wabunge, vipi sasa Dk Mashinji? Mbona yeye sio mbunge naye hana sifa za kuwa wakala?
Shahidi: Ndio hana sifa kwa sababu mawakala wote wanaosimamia uchaguzi lazima wale kiapo, hivyo Dk Mashinji hakuwepo katika kiapo na wala hakula kiapo.
Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni wabunge; Esther Matiko (Tarime Mjini); Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini); Halima Mdee (Kawe), John Heche (Tarime Vijijini), John Mnyika (Kibamba), Ester Bulaya (Bunda Mjini) pamoja na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji na Salum Mwalimu ambaye ni Naibu Katibu Mkuu- Zanzibar.
Washitakiwa hao wanakabiliwa na makosa 13 likiwemo la kula njama, ambapo wote wanadaiwa kuwa, Februari 16, 2018, Dar es Salaam waliku?a njama ya kutenda kosa la kufanya mkusanyiko usio halali na kukiuka tamko kutawanyika.
Kesi bado inaendelea mahakamani, endelea kufuatili Mwananchi kwa habari zaidi