Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Samia atamba na CCM yake

Samia Ccm.jpeg Samia atamba na CCM yake

Mon, 6 Feb 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Samia Suluhu Hassan amekipongeza chama hicho kwa kutimiza miaka 46.

“Pongezi kwa wana CCM na Watanzania wote. Busara na maono ya waasisi wetu viliunganisha TANU na ASP kutujengea chama hiki chenye misingi imara, kinachoendelea na kazi adhimu ya kuwatumikia Watanzania, Awamu hadi Awamu”aliandika Rais Samia jana kwenye ukurasa wake katika mtandao wa kijamii wa twitter.

CCM ilianzishwa mwaka 1977 kwa kuunganisha vyama vya Tanganyika African National Union (TANU) na Afro Shiraz Party (ASP).

Mlezi wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Philip Mpango aliwataka viongozi chama hicho kutoka na kwenda kusikiliza kero na matatizo ya wananchi badala ya kukaa ofisini kwani hiyo siyo tabia ya viongozi wa CCM.

Dk Mpango alisema hayo katika viwanja vya Mnazi Mmoja jana alipozungumza na wafuasi wa wa chama hicho wakati wa maadhimisho ya miaka 46 ya kuzaliwa kwa chama hicho.

“Viongozi wa Chama cha Mapnduzi, ni chama cha wanyonge cha kusemea watu kwa hiyo nawaomba viongozi wa maofisini siyo wa CCM, mtoke mkaongee na wananchi, mkawasikilize shida zao na kuzitatua,” alisema.

Dk Mpango aliwahimiza wajenge tabia ya kutoka nje ya ofisi na kwenda kusikiliza na kuwahudumia wananchi pamoja na watumishi wa umma walio chini yao huku akimsisitiza Mwenyekiti wa mkoa asichoke kuwasikiliza wananchi na kutatua kero zao.

Pia alieleza umuhimu wa wananchi kulipa kodi kwa maendeleoya taifa na kuwasisitiza viongozi wa chama washirikiane na serikali kutoa elimu na kuhimiza raia kulipa kodi ili iweze kuendelea.

Dk Mpango alisema hakuna nchi inayoendelea kwa mapato ya kupewa na nchi nyingine na badala yake kila nchi huendelea kwanza kwa mapato ya ndani kabla ya kugeukia vyanzo vya nje hivyo ni lazima nchi isimame yenyewe kwa kukusanya kodi ikiwemo kodi kutoka katika vyanzo vya Halmashauri.

“Ni lazima tusimame wenyewe, lakini pia katika Halmahsuri zetu mnafanya vizuri lakini muendelee kusimamia na mzidi kufanya vizuri zaidi,” alisema.

Aidha Dk Mpango alizungumzia kuimarika kwa demokrasia nchini na kusema kuwa kwa sasa demkorasia ya nchi kupitia Rais Samia Suluhu Hassan imeimarika kwani amefanikiwa kuweka mazingira mazuri katika eneo hilo huku akimwelezea kuwa amejipambania kama mwalimu mzuri katika kuvumiliana na kuishi kwa umoja.

Alisema jambo hilo lilionekana wazi aliporuhusu mikutano ya kisiasa na kuwataka wanasiasa kutumia nafasi hiyo vizuri kwa kufanya siasa za kistaarabu kwani kuitumia vibaya nafasi hiyo, ni kuchelewesha maendeleo ya nchi

Dk Mpango alisema hakuna sababu za wanasiasa kugombana bali watumie mikutano kujadiliana kwa hoja badala ya kuendekeza maandamano yasiyo na msingi ili Tanzania iendelee kupaa kimaendeleo.

Katika tukio hilo pia alikabidhi kadi kwa wanachama wapya 580 akiwemo Dk Mayrose Majinge aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa UVCCM wilaya ya Ilala ambaye alirejea CCM akitoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Mbali na hayo Dk Mpango alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makala aendelee kutilia mkazo usalama wa mkoa ikiwa ni pamoja na kutokomeza tishio la kundi la wahalifu la panya road.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live