Rais Samia Suluhu Hassan amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, Balozi Pindi Chana kuandaa kanuni zitakazoelekeza jinsi ya kufanya mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa.
Alitoa maelekezo hayo baada ya kupokea maazimio ya awali kutoka kikosi kazi alichokiteua cha kufuatilia hoja zilizojitokeza katika mkutano wa wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa uliofanyika jijini Dodoma kuanzia Desemba 15 hadi 17 mwaka jana.
Rais Samia alimuagiza Waziri huyo kushirikiana na Tanganyika Law Society (TLS) pamoja na Zanzibar Law Society (ZLS) kutengeneza kanuni hizo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, kikosi kazi hicho chenye wajumbe 24 na ambacho kinawajibika moja kwa moja kwa Rais, kiliwasilisha maazimio hayo Ikulu, jijini Dodoma. Maazimio hayo yamegawanyika katika makundi matatu ya muda wa utekelezaji.
Alisema azimio la muda mfupi ni uandaaji wa kanuni zitakazoelekeza jinsi ya kufanya mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa.
“Baadhi ya maazimio ya muda wa kati ni pamoja na rushwa na maadili katika uchaguzi, ruzuku, elimu ya uraia, huku masuala yanayohusu uchaguzi na katiba mpya vikiwa ni mpango wa muda mrefu,” alisema.