Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Umma (Chauma), Hashimu Rungwe amesema Tanzania bado inahitaji katiba mpya licha ya mchakato wake kukwama mwaka 2014 kupisha uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Rungwe ameyasema hayo leo Alhamisi Machi 12, 2020 katika ofisi za kampuni ya Mwananchi Communications Ltd( MCL) zilizopo Tabata Relini jijini Dar es Salaam. MCL inachapisha magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti.
Akizungumza katika mahojiano na wahariri na waandishi wa MCL, Rungwe ambaye mwaka 2010 aligombea urais kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi amesema, “Ule mchakato tulienda nao bungeni (Bunge Maalum la Katiba) lakini kwa kuwa ulikuwa unategemea majority (wingi) wenzetu wa chama tawala (CCM) walikuwa wengi hivyo walishinda katika mchakato ule.”
“Wenzetu pamoja na wengi wao wameshindwa kumaliza mchakato huu hatujui sababu za kuchelewa wakati tuliambiwa kuwa katiba imeshakamilika ila ukweli ni kwamba katiba mpya ni muhimu sana.”
Rungwe pia aligusia suala la kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara akidai kumechangia vyama kukosa mvuto kwa wananchi.