NAIBU Waziri wa Ardhi, Ridhiwan Kikwete ameahidi kushughulikia tatizo la mgogoro wa ardhi kwenye eneo la Chasimba, Bunju wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na HabariLeo, Ridhiwan amesema tayari amekutana na Mbunge wa Kawe, Joseph Gwajima na kuzungumzia kwa undani mgogoro huo ambao umeibuka upya kwa wakazi wa maeneo hayo kugoma kulipa tozo ya skwea mita na badala yake wanataka kulipa tozo ya Primer kama walivyokubaliana katika kikao cha March 14, 2021 chini ya aliyekuwa Waziri wa Ardhi wa wakati huo Wiliam Lukuvi.
“Nimekutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Joseph Gwajima kujadili mvutano pale Chasimba, nimemuahidi kufuatilia na kutatua changamoto zilizopo.” Amesema
Kauli ya Ridhiwan imekuja baada ya wananchi wa Chasimba kuandamana mwishoni mwa wiki wakimuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuingilia kati madai yao ambayo wanadai kukiukwa kwani katika makubaliano yao na Waziri wa Ardhi wa wakati huo na watendaji wa Manispaa ya Kinondoni walitakiwa kupima ardhi na kulipa tozo ya premier lakini kwa sasa wanadai kutakiwa kulipa tozo ya Skwea mita ambayo ni shilingi shilingi 6,416.