Dodoma. Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa amemtaka Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango na Profesa Palamagamba Kabudi wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kujiuzulu kwa kuwa wanamshauri vibaya Rais John Magufuli kuhusu masuala mbalimbali ya uchumi.
Akizungumza leo Jumatatu Juni 17, 2019 katika mjadala wa bajeti kuu ya Serikali ya Sh33.1 trilioni bungeni jijini Dodoma, Mchungaji Msigwa amesema mawaziri hao wapo karibu zaidi na Magufuli, kwamba licha ya wapinzani na wabunge kushauri kuhusu masuala mbalimbali ya uchumi tangu mwaka 2016, wawili hao walishindwa kumshauri kiongozi mkuu huyo wa nchi.
Mchungaji Msigwa amemtaja Profesa Kabudi kumshauri vibaya Rais Magufuli kuhusu masuala ya madini na kusababisha sekta hiyo kukwama na Dk Mpango kutoa ushauri usiofaa katika masuala ya uchumi.
“Niliwahi kusema ukiwa unakimbia mwendo kasi na umepotea njia ule mwendo kasi hauna maana. Ni miaka minne sasa hapa bungeni tunajadili kuhusu maendeleo ya nchi yetu, kuhusu malalamiko bandarini, masuala ya utalii na hata kukusanya kodi kwa bunduki. Leo baada ya miaka minne mmebadili lugha na kuwa laini kama si nyinyi.”
“Hivi ule ushauri tuliowapa kipindi kile kwanini mlikuwa mnakataa mlitaka kupata nini? sasa hivi mnatekeleza yale yale baada ya kuliingiza Taifa katika matatizo,” amehoji Mchungaji Msigwa.
Amesema Dk Mpango tangu awe waziri wa wizara hiyo, makamishna mbalimbali wa taasisi zilizo chini ya wizara ya Fedha na Mipango wanaondolewa jambo linaloashiria kuwa ameshindwa kuongoza.
Pia Soma
- Mbunge CUF ataka Bunge lichunguze ukweli wa mgawanyo wa mapato
- Wapinzani Tanzania waja na bajeti ya Sh 29 trilioni, vipaumbele vitano
- CTI yaimwagia sifa Serikali ya Tanzania
“Wananchi wanataka kuona maisha yao yanakwenda. Nyinyi ndio mnaomshauri rais zaidi kuhusu masuala ya uchumi sasa mnafanya nini,” amesema Mchungaji Msigwa.