Iringa. Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda amewataka wajumbe wa mkutano mkuu maalum wa CCM Mkoa wa Iringa kuchagua kiongozi anayepiga vita makundi.
Pinda ambaye ni mlezi wa CCM Mkoa wa Iringa ametoa kauli hiyo leo Jumapili Januari 6, 2018 katika mkutano huo wa kumchagua mwenyekiti wa chama hicho tawala mkoani Iringa.
“Hapa tunahitaji kiongozi ambaye hataendeleza makundi. Mtu mwenye msimamo atakayeweza kukemea ukabila na ukanda. Kiongozi atakayewaunganisha wananchi na Serikali huyo tumpe,” amesema Pinda.
Amesema ikiwa wajumbe wa mkutano huo wataona hakuna mgombea mwenye sifa ni vyema karatasi za kura wasijaze kitu
“Kama mgombea amepita na kugawa fedha ili umchague achana naye maana hatufai. Huyo hatakuwa na uwezo wa kuongoza bila rushwa. Tupo kupambana kuzuia matumizi mabaya ya fedha. Huyo mgombea hatufai msimchague ili awamu ijayo ajifunze,” amesema.
Aliyekuwa mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Albert Chalamila amewataka wajumbe wa mkutano huo kuchagua kiongozi bora na si kumbagua kwa misingi waliyonayo.
“Wapo wajumbe wanambagua mgombea Amani Mwamwindi kwa udini ila wanambagua Vitus Mushi kwa ukabila na Abel Nyamhanga kuwa si mzoefu. Hiyo yote si misingi ya chama,” amesema Chalamila.