Mirerani. Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda amewapokea wanachama wapya wa upinzani 233 akiwemo aliyekuwa Katibu wa Chadema wilayani Simanjiro na mwenyekiti wa vijana (Bavicha) Mkoa wa Manyara, Frank Oleleshwa.
Wanachama hao wa Chadema wamepatiwa kadi za CCM na Pinda katika ziara yake ya siku nane Mkoa wa Manyara.
Akizungumza leo Alhamisi Machi 21, 2019 kwa niaba ya wanachama wenzake, Oleleshwa amesema sababu za kuhamia CCM zipo nyingi ila yale aliyokuwa anapigania alipokuwa Chadema yanafanyika CCM.
"CCM imeonyesha utashi mkubwa wa uzalendo katika kuongoza nchi hivyo tumeamua kuhamia huku ili kuunga mkono juhudi hizo," amesema Oleleshwa.
Akizungumza baada ya kuwakabidhi kadi wanachama hao wapya wa sehemu mbalimbali wilayani Simanjiro, Pinda aliwapongeza kwa kujiunga na CCM.
Pinda amesema hivi sasa Rais Magufuli anafanya kazi kubwa ya kufanikisha maendeleo hivyo Watanzania wanapaswa kumuunga mkono.