Dodoma. Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda, amemmwagia sifa mbunge wa Dodoma Mjini, Anthony Mavunde kuwa ni miongoni mwa vijana wanaofanya kazi ya kuridhisha.
Hiyo itakuwa ni bahati kwa mwanasiasa huyo kijana ambaye ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Vijana), kusifiwa na mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambayo inasimamia uteuzi wa wagombea.
Juzi, Pinda alitoa sifa hizo mbele ya katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally kwenye mkutano wa wanachama wakizindua miradi ya uwekezaji kwa chama.
Pinda alimsimamisha Mavunde mbele ya Dk Bashiru na kueleza kuwa anastahili kuungwa mkono katika kazi za siasa ndani ya jimbo hilo, huku akimpigia debe kuwa ikiwezekana angeachwa kuendelea na kazi hiyo kwanza.
Hata hivyo, Pinda alisema chama hicho hakitakuwa tayari kuwavumilia watu ambao wanaonekana hawawezi kukisaidia na kukivusha kwenye uchaguzi huki akiomba mkoa kumpa nafasi ya kufanya ziara ili kukagua uhai wa chama.
Naye Dk Bashiru aliwaomba wanachama kuacha kubadilisha uongozi kwa ushabiki badala yake, wawaondoe wasiofaa ambao hata wakishinda kura za maoni chama kinawajua watakatwa.
Pia Soma
- Rais apiga Marufuku kuimba wimbo wa Taifa
- Sampuli za mabaki ya Naomi zatua kwa mkemia mkuu
- UCHOKOZI WA EDO: Mlevi aliyesubiri majibu ya Rais kuhusu ‘Clip’
Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dodoma, Godwin Mkwanwa alisema mkoa huo ndiyo ngome ya CCM hivyo wamejiandaa kikamilifu kuanzia uchaguzi wa serikali za mitaa.