Monduli. Mbunge wa zamani wa Longido (Chadema), Onesmo ole Nangole leo Jumamosi Machi 9, 2019 amerejea CCM pamoja na wafuasi wengine waliokuwa upinzani zaidi ya 30 katika hafla ya kumpokea Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.
Nangole ambaye alikuwa mwenyekiti wa CCM mkoa wa Arusha na kujiuzuru mwaka 2015 na kujiunga na Chadema na baadaye, kugombea ubunge jimbo la Longido, amesema amerejea CCM nyumbani.
"Kama ulivyoona nimerejea CCM, lakini nitazungumza sababu nyingi ambazo zimenifanya kurejea CCM," amesema
Wengine ambao walijiunga na CCM ni wanachama wa upinzani katika maeneo mbalimbali ambao hata hivyo sasa inawapasa kufuata taratibu za kujiunga na CCM kupitia katika ofisi
Akizungumza baada ya kuwapokea wanachama wapya, Katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Hamphrey Polepole amewataka kufuata taratibu za kujiunga na CCM kama ambavyo amefanya Lowassa.
Amesema Lowassa amefuata taratibu zote ambazo zilipaswa ili kupokelewa na CCM na akawataka ambao wanarejea CCM kufuata taratibu.
Akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Arusha, Loata Sanare amesema wanamkaribisha sana Lowassa nyumbani na kueleza wangemshangaa sana kama angeendelea kubaki chadema.
Amesema Lowassa amerudi katika chama baada kufuata taratibu na wanamshukuru kwa kurudi CCM chama ambacho ndicho kimemlea na chama ambacho ndicho ameacha marafiki zake wengi.
Sanare amesema wale wote waliokwenda upande wa pili wa upinzani lazima wafuate utaratibu, kama Lowassa, kwani Lowassa licha ya kupokelewa na Mwenyekiti wa CCM Taifa lakini aliandika barua kwenye tawi lake.
"Wote ambao mnataka kurudi CCM fateni utaratibu kuomba uanachama upya katika maeneo yenu...Lowassa karibu sana CCM tunaamini na wewe uliimiss sana CCM karibu sana" alisema