Dar es Salaam. Vyama vya siasa nchini Tanzania vitakavyokumbana na changamoto wakati wa chaguzi ndogo vimetakiwa kupeleka malalamiko yao kwenye kamati za maadili.
Endapo wakishindwa kufanya hilo malalamiko yao hayawezi kufanyiwa kazi kwa kuwa kamati hizo za maadili ndizo zenye jukumu hilo.
Hayo yameelezwa leo Jumatano Juni 19,2019 na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Uchaguzi (NEC) Dk Athuman Kihamia wakati watendaji wa tume hiyo walipokutana na wahariri wa vyombo vya habari.
Amesema uzoefu unaonyesha kamati hizo zimekuwa hazipelekewi malalamiko na badala yake vyama vinakimbilia kwenye vyombo vya habari.
“Ukipeleka malalamiko kwenye vyombo vya habari hayawezi kufanyiwa kazi kwa sababu jukumu la kushughulikia hayo lipo kwenye kamati za maadili,” amesema
Kufuatia hilo Dk Kihamia amesisitiza vyama vya siasa na wanasiasa wenye malalamiko kuyapeleka kwenye kamati hizo ili yafanyiwe kazi.