Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

NEC yatangaza nafasi wasimamizi uchaguzi Konde

Kuraaa.png Tume ya Taifa ya Uchaguz ( NEC )

Thu, 2 Sep 2021 Chanzo: MWANANCHI

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza nafasi ya msimamizi wa uchaguzi jimbo la Konde pamoja na wasimamizi wasaidizi wawili watakaokuwa na jukumu la kusimamia uchaguzi mdogo wa jimbo hilo unaotarajiwa kufanyika Oktoba 9, 2021.

Agosti 2, 2021 NEC ilitangaza jimbo hilo kuwa wazi baada ya aliyechaguliwa kuwa mbunge katika uchaguzi wa Julai 18, 2021, Sheha Mpemba Faki kujiuzulu akidai kutishiwa maisha pamoja na familia yake.

Uchaguzi katika jimbo hilo ulifanyika baada ya kifo cha Khatib Said Haji aliyeibuka mshindi katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 28, 2020.

“Kila mwombaji katika nafasi husika aainishe nafasi anayoiomba na aambatanishe maelezo ya taarifa binafsi akiweka jina la taasisi anayofanyia kazi na cheo chake. Mwisho wa kupokea maombi ni Septemba 3, 2021,” linaeleza tangazo hilo lililosainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi (NEC), Dk Wilson Mahera.

Akifafanua hatua ya NEC kutangaza nafasi hizo, mkurugenzi wa idara ya habari na elimu ya mpiga kura wa tume hiyo, Giveness Aswile amesema muundo wa utawala wa Zanzibar ni tofauti na Tanzania Bara ambako wamekuwa wakiwatumia wakurugenzi wa halmashauri.

Amesema katika chaguzi zote za Zanzibar wamekuwa wakitangaza nafasi hizo na wanaotakiwa kusimamia uchaguzi ni miongoni mwa watumishi wa umma ambao wana sifa za kusimamia uchaguzi.

“Hii sio mara ya kwanza kutangaza, ni miaka yote kwa upande wa Zanzibar hakuna halmashauri, hamna wakurugenzi wa halmashauri, kwa hiyo huwa tunatangaza lakini bado tunachukua watumishi wa umma,” amesema Aswile.

Akizungumzia suala hilo, katibu wa habari, uenezi na mahusiano na umma wa ACT Wazalendo, Salim Bimani amesema kisheria NEC wanatakiwa kutangaza nafasi za wasimamizi lakini hawatangazi bali wanaweka watu wao.

Amesema hilo halikufanyika kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka jana, pia halikufanyika kwenye uchaguzi mdogo wa Julai 18, 2021 jambo linalowasukuma kuwasilisha malalamiko yao tume kuhusu uchaguzi huo.

“Huu ni utaratibu ambao tume wanatakiwa waufanye lakini hawafanyi. Sisi baada ya uchaguzi wa Konde tuliwaandikia tume barua kuonyesha zile kasoro zilizojitokeza Konde na kuwataka wafanye uandilifu, watangaze hizo nafasi,” amesema Biman

Chanzo: MWANANCHI