Dar es Salaam. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza ratiba ya uchaguzi mdogo wa ubunge wa Singida Mashariki kuwa utafanyika Julai 31 mwaka 2019.
Uchaguzi huo unafanyika ili kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Tundu Lissu ambaye Julai 28 mwaka 2019, Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai alilitangazia Bunge hilo kuwa Lissu amepoteza sifa za kuwa mbunge akitoa sababu mbili.
Spika Ndugai alisema Lissu hajajaza fomu za mali na madeni za maadili kwa viongozi wa umma pamoja na kutokutoa taarifa kwake (spika).
Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa Julai 05, 2019 na Mwenyekiti wa NEC Jaji Semistocles Kaijage amesema kutokana na barua ya Spika Ndugai kuwa Lissu kapoteza sifa ya kuwa mbunge kutokana na kushindwa kuwasilisha kwa Spika tamko la mali na madeni na kushindwa kuhudhuria mikutano saba mfululizo ya Bunge bila ruhusa ya Spika.
Jaji Kaijage amesema Spika Ndugai alizingatia matakwa ya kifungu cha 37 (1) (b) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi sura ya 343, kutoa taarifa kwa Umma kuhusu uwepo wa Uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Singida Mashariki.
Amesema kwa kuzingatia Katiba ya nchi na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, ratiba ya uchaguzi huo utakuwa ni fomu za uteuzi wa wagombea zitatolewa kati ya Julai 13 hadi 18 mwaka 2019.
Pia Soma
- Waziri wa Misri aahidi ushirikiano ujenzi mradi wa umeme Rufiji
- Uvamizi waporomosha Tanzania vivutio vya asili
- Tanapa yatumia Sh1.7 bilioni kupanga matumizi bora ya ardhi na kutatua migogoro
Mwenyekiti huyo alivikumbusha vyama vya Siasa na wadau wote wa uchaguzi kuzingatia Sheria, Kanuni, Maadili ya Uchaguzi, Taratibu, Miongozo na Maelekezo yanayotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi wakati wa kipindi chote cha uchaguzi huu mdogo.