Arusha. Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha, Lootha Sanare amesema mkoa huo haukumuunga mkono Rais John Magufuli katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 lakini baada ya kuona utendaji wake, umekuwa wa kwanza kujutia jambo hilo.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Julai 27, 2019 katika kongamano la Umoja wa Wanawake (UWT) kumpongeza Rais Magufuli kwa kutekeleza ilani ya uchaguzi ya chama hicho mwaka 2015-2020.
Amesema baada ya uchaguzi huo CCM ilipata mbunge mmoja kati ya saba wa Mkoa wa Arusha lakini hivi sasa chama hicho tawala kina wabunge wanne na kuvuna madiwani 72 waliojiunga nacho wakitokea Chadema.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amesema kasi ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Magufuli imeendelea kuleta mabadiliko katika sekta ya afya, barabara, elimu na utalii.
"Kabla ya kuwapata hawa wabunge Monduli, Longido na Arumeru Mashariki tulikua na mbunge mmoja tu wa Ngorongoro,William Ole Nasha. Kwa hiyo wabunge wa viti maalumu walitusaidia sana naomba tuwapongeze Catherine Magige na Amina Mollel," amesema Gambo.
Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Arusha, Jasmin Bachu amesema katika uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Oktoba, 2019 mitaa na vijiji vyote vitakua vya kijani.
Pia Soma
- Trump atangaza kodi kwa bidhaa za Ufaransa
- Halima Bulembo awataka vijana kutokata tamaa
- Diamond atajwa mkutano mkuu wa NCCR-Mageuzi
Baadhi ya viongozi waliohudhuria ni naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha; naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo Makazi, Angela Mabula; naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Dk Mary Mwanjelwa; naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia walemavu, Stella Ikupa.