Monduli. Mbunge wa Geita Vijijini (CCM), Joseph Kasheku ‘Musukuma’ amewataka wakazi wa kata ya Mto wa Mbu kumchagua Julius Kalanga kuwa mbunge wa Monduli ili eneo hilo kupata hadhi ya kuwa mamlaka ya mji mdogo.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni za uchaguzi zilizofanyika katika kata hiyo leo Jumamosi Septemba Mosi, 2018, Musukuma amesema Mto wa Mbu ina sifa ya kuwa mji mdogo.
“Mchagueni Kalanga tutashirikiana nae ili hapa pawe mamlaka ya mji mdogo, kwani mnakosa nini,” amesema na kuwataka mamia ya wananchi waliojitokeza kubadilika kwa kuwa sasa Kalanga anagombea akiwa CCM.
Kalanga alikuwa mbunge wa Monduli kwa tiketi ya Chadema kuanzia 2015 hadi Julai 31, 2018 alipohamia CCM ambako amepitishwa kuwania tena ubunge katika jimbo hilo.
Kwa upande wake Kalanga amesema anajua shida za Mto wa Mbu na hata kabla ya kujiunga na CCM alikuwa akifika kuwasikiliza wananchi.
Amesema wakimchagua atahakikisha eneo hilo linakuwa na stendi ya mabasi na soko la kisasa la ndizi.