Pemba. Leo mchana Alhamisi Januari 30, 2020 mshauri mkuu wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad amechukua fomu za kugombea uwenyekiti wa chama hicho jambo ambalo limewaibua watu wa kada mbalimbali na kutoa maoni tofauti kuhusu uamuzi wake huo.
Wakizungumza na Mwananchi, Aley Massoud Aley amesema amekua akimfahamu Maalim Seif kama mwanasiasa anayejua mbinu za mapambano na amekuwa mwiba kwa chama tawala.
Amesema uamuzi wake wa kuchukua fomu utawafanya wananchi wengi kuamua kujiunga na chama hicho.
Aley amesema baadhi ya wananchi waliamua kubaki CUF wakiamini kuna siku Maalim Seif wangebadili uamuzi na kurejea katika chama hicho.
Aisha Seleman amesema Maalim Seif atabaki kuwa shujaa wao kwa kuwa hakuna mwingine wa kumuamini.
Amesema uamuzi wake wa kuchukua fomu umeibua matumaini na kwamba ana amini katibu mkuu huyo wa zamani wa CUF atachukua fomu za kugombea urais Zanzibar.