Mbunge wa Singida Mashariki, Miraji Mtaturu amesema kipaumbele chake cha kwanza jimboni humo ni kuhakikisha kila mtoto anapata elimu kwakuwa elimu ndio msingi wa maendeleo kwenye kada yoyote hapa nchini.
Mtaturu amesema hayo jimboni humo alipokuwa anatoa vifaa mbalimbali vya masomo kwa wanafunzi 1161 wanaotoka katika familia zisizo na uwezo.
“Serikali yetu imewekeza katika elimu ambayo kwa sasa ni bure na mimi kama mbunge naunga mkono jitihada hizi za serikali kwa kutoa vifaa vya shule ili kisiwepo kikwazo chochote kwa watoto ambao wazazi wao hawana uwezo” amesema Mtaturu.
Vifaa alivyotoa mbunge huyo ni pamoja na sare za shule, madaftari pamoja na kalamu vyenye thamani ya shilingi milioni 30.