Dar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF, Julius Mtatiro ametangaza kujiondoa kwenye chama hicho leo Agosti 11.
Akizungumza na wanahabari leo, Mtatiro amesema ametafakari kwa miaka zaidi ya kumi aliyofanya siasa na kuona kwamba umefika wakati wa kuunga mkono juhudi za Rais John Magufuli.
“Masuala ya misimamo yangu ya sera na ilani ya CUF na misimamo ya CUF hayo yanabaki CUF, hivi sasa mimi ni Mtatiro ambaye ninajiandaa kuhamia CCM, kama mwananchi ninayo haki kikatiba,”amesema.
Amesema amejiridhisha kwa hitaji ya nafasi yake kwamba ajiunge na CCM na akasema anawajulisha watanzania kuwa ameanza mipango ya kutekeleza hilo mara moja.
Amesema hajanunuliwa wala kurubuniwa na CCM bali ameitumia siku ya leo kuonyesha nia yake ya kuhamia CCM na kuomba wampokee.