Zanzibar. Msimamizi Uchaguzi Jimbo la Jang’ombe, Mwanapili Khamis Mohamed amesema shughuli ya upigaji kura imeanza vyema kama ilivyopangwa na Tume ya Uchaguzi.
Akiwa katika kituo kidogo cha kupigia kura Shehia ya Jang’ombe leo asubuhi Mwanapili alisema hakukuwa na malalamiko yoyote juu ya uendeshaji wa uchaguzi huo.
Alisema kwa mujibu wa utaratibu shughuli ya upigaji kura ilianza saa 1:00 asubuhi japokuwa idadi ya wananchi waliojitokeza ni ndogo kwa wakati huo.
Alisema matumaini yao kuwa idadi ya wapiga kura itaongezeka kadri muda unavyoenda.
Mwanapili alitoa wito kwa wapiga kura jimboni humo kuendelea kujitokeza kwa wingi ili kutumia fursa ya kumchagua kiongozi wanayemtaka.
Baadhi ya wapiga kura waliojitokeza walionyesha kuridhishwa na utaratibu ulioandaliwa na tume hiyo kwa kuweka wasimamizi wa kutosha.
Mmoja wa wapiga kura hao, Simai Muhamed Simai alisema utaratibu huo pia unahitajika kufanywa katika uchaguzi mkuu.