Dodoma. Dk John Pallangyo ameapishwa leo Jumatano Mei 22, 2019 kuwa mbunge wa Arumeru Mashariki (CCM) kuchukua nafasi ya Joshua Nassari (Chadema) aliyepoteza sifa za kuwa mbunge.
Dk Pallangyo ameapishwa na Spika wa Bunge, Job Ndugai huku wabunge wa CCM wakimsindikiza kwa mbwembwe na kuimba nyimbo za CCM, wakati wakimsindikiza.
Mara baada ya kuapishwa alikwenda kusalimiana na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi na Wenye Ulemavu.
Baadaye alihamia upande wanapokaa wapinzani na kusalimiana na Kaimu Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Joseph Selasini na Mbunge wa Kibamba (Chadema), John Mnyika ambao kwa pamoja waliteta kidogo kama sekunde kadhaa.
Kisha mtumishi wa Bunge alimpeleka eneo ambalo atakuwa akikaa.
Dk Pallangyo amechukua nafasi hiyo baada ya Nassari kupoteza fursa hiyo kwa kutohudhuria vikao vya mikutano mitatu ya Bunge mfululizo pasina kutoa taarifa kwa ofisi ya Spika.
Pia Soma
- Mfuko mdogo wa plastiki kukuweka jela siku saba, faini ya Sh30,000
- Mbunge: Wanawake wanaozurura mtaani wapelekwe JKT kufanya kazi
- Wabunge 7 Chadema kuvuliwa nyadhifa
- MWANANCHI JUKWAA LA FIKRA: Rukwa na Katavi sasa wageukia kilimo cha kisasa kutoka kilimo cha mazoea
Tofauti na wabunge waliohama upinzani na kisha kupitishwa na CCM kugombea, walipokuwa wakiapishwa, wabunge wa upinzani walikuwa wakitoka na kutoshuhudia kiapo lakini leo wabunge wa upinzani wamebaki na kushuhudia kiapo hicho.