Dar es Salaam. Mgombea ubunge wa Ukonga (Chadema), Asia Msangi amechukua fomu kuwania nafasi hiyo.
Asia amechukua fomu jana Agosti 16, 2018 katika ofisi za Halmashauri ya Ilala jijini Dar es Salaam.
Katika uchaguzi wa jimbo hilo utakaofanyika Septemba 16, 2018, Msangi atachuana na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Mwita Waitara aliyetimkia CCM na kupitishwa kugombea tena.
Akizungumza na MCL Digital leo Ijumaa Agosti 17, 2018, Msangi amesema, “ninachokifanya sasa ni kuijaza kisha kuirejesha kwa hatua nyingine.”
Kuhusu kuchuana na Mwita amesema, “kama ambavyo chama kimeniamini nitautunza uaminifu huo na yale ambayo Chadema iliyaahidi mwaka 2015 nitakwenda kuyatekeleza.”
“Mwita hafai kuwa kiongozi kwani amewasaliti wana Ukonga, kwa hiyo atakwenda kupata malipo yake kutoka kwa wana Ukonga waliomwamini mwaka 2015.”
Mwenyekiti wa Chadema wilaya ya Ilala, Dk Makongoro Mahanga amesema baada ya kuwa amechukua fomu, kinachofanyika ni kuijaza na Jumatatu Agosti 20, 2018 atairudisha.