Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mkumbo: Chagua CCM kuleta maendeleo, acha uanarakati

9a965bfd3041590d6b5701f81df38782 Mkumbo: Chagua CCM kuleta maendeleo, acha uanarakati

Thu, 1 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MGOMBEA ubunge wa Jimbo la Ubungo kupitia Chama Cha Mapindunzi (CCM), Profesa Kitila Mkumbo amewataka wananchi wa jimbo hilo kuchagua maendeleo dhidi ya uanaharakati ili wapate huduma zilizo bora ikiwemo miundombinu ya barabara.

Profesa Mkumbo aliyasema hayo wakati wa kampeni zake katika eneo la Sinza Palestina jijini Dar es Salaam juzi ambapo aliwataka wananchi wa Sinza wasirudie makosa waliyoyafanya mwaka 2015.

“Kuna kuchagua maendeleo na kuchagua uanaharakati, hivi ukichagua mtu anayenadi harakati unategemea nini jamani? Lazima maendeleo yatachelewa tu! Ndiyo sababu mpaka leo wananchi wa Sinza mnateseka na suala la barabara,” alisema.

Aliwataka wananchi wa Ubungo wachague watu watakaounda Serikali Kuu na Serikali za Mitaani zilizo imara zenye uwezo wa kuwaletea maendeleo huku akiongeza kuwa hana shaka na Rais John Magufuli katika kuunda Serikali Kuu.

“Rais Magufuli ni mtu sahihi kwa upande wa Serikali Kuu, wenyewe mnaona miundombinu ya reli na barabara iliyopo katika jimbo letu, tatizo liko katika serikali za mitaa zinazoundwa na wabunge na madiwani, msifanye makosa tena, chagueni wagombea wa CCM mpate maendeleo, haiwezekani Serikali Kuu iundwe na CCM, Serikali za mitaa ziundwe na upinzani,”alisema.

“Mwaka 2015 mliwapa wapinzani Serikali za Mitaa zikaundwa na madiwani na wabunge wa upinzani matokeo yake Serikali Kuu ikatekeleza wajibu wake lakini Serikali za mitaa changamoto zinaonekana ikiwemo uchafu kwenye masoko na miundombinu duni ya barabara za kwenye mitaa zikiwemo hizi za mitaa ya Sinza zilizojaa mashimo,”alisema.

Alisema mgombea anayeweza kuleta maendeleo kwa wananchi ni yule mwenye uwezo wa kushawishi Serikali Kuu na yeye anao uwezo huo kwa sababu amefanya kazi na Serikali Kuu kwa miaka mitatu na ameshiriki katika kutatua baadhi ya kero za wananchi wa Ubungo ikiwemo tatizo la upatikanaji wa maji.

“Hakuna mgombea anayeweza kuleta maendeleo kwa fedha ya mfukoni mwake, ni mlazima mgombea aeleze namna atavyopata fedha hizo. Mimi nimepiga hesabu ya makusanyo ya Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo ni Sh bilioni mbili kwa mwezi.

“Nitaomba tutenge asilimia tano sawa na milioni 100 ziende kwenye mfuko wa barabara na fedha nyingine zitatoka kwenye mfuko wa jimbo lakini ili hayo yafanikiwe, ni vema mrudishe uongozi wa CCM kwa kumchagua Raphael Awino kuwa diwani wenu na mimi kuwa mbunge wenu,”alisema.

Aliahidi kusimamia malipo ya fidia kwa walioathiriwa na ujenzi wa kingo za mto ng’ombe, kusimamia masuala ya michezo kwa vijana ikiwa ni pamoja na ujenzi wa viwanja vya michezo na kusimamia uboreshaji wa mfumo wa utoaji mikopo kwa wanawake.

Pia aliahidi kusimamia uboreshaji wa sekta ya elimu kwa kuboresha mazingira ya utendaji kwa walimu na kujenga uzio katika shule za Jimbo hilo kwa ajili ya usalama wa wanafunzi

Chanzo: habarileo.co.tz