MGOMBEA udiwani, Kata ya Kabwe iliyoko mwambao mwa Ziwa Tanganyika wilayani Nkasi katika Mkoa wa Rukwa, Asante Lubisha kupitia tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) amesema akichaguliwa tena atapigania serikali iwaruhusu wakazi wa kata hiyo kuanzisha mabucha ya kuuza nyama ya mamba na viboko ikiwa ni namna ya kuwavuna wanyama hao.
Alisema kuwa wanyama hao wamezaliwa kwa wingi na kusababisha taharuki kubwa kwa wakazi wa kata hiyo ambao wanashindwa kufanya shughuli za kilimo na uvuvi wakihofia kushambuliwa na wanyama hao.
Mwanasiasa huyo ambaye anaomba ridhaa ya kuchaguliwa tena katika mhula wake wa nne alilieleza HabariLeo katika mahojiano yaliyofanyika kwa njia ya simu juzi.
Alisisitiza kuwa tangu achaguliwe kwa mara ya kwanza hadi sasa watu 25 wameshambuliwa na mamba kati yao 15 wameliwa na wanyama hao huku waliojeruhiwa wakiwa 10.
“Kwa sababu tayari serikali ya CCM imesharuhusu raia kuanzisha mabucha ya wanyamapori basi nikichaguliwa tena nitawasiliana na Mamlaka husika ili wananchi wa kata hii au kutoka nje waruhusiwe kuanzisha mabucha ya kuuza nyama ya viboko na mamba...wanyama hawa wamezaana sana, ni tishio kubwa kwa maisha ya wananchi.
Njia ya kuwavuna ni wananchi washawishike kuanzisha mabucha hayo wakifuata sheria, kanuni na taratibu ambazo tayari zimewekwa wazi na serikali,” alieleza.