Dar es Salaam. Mgombe udiwani wa Vingunguti (CUF), Hamadi Faki amedai takribani zaidi ya mawakala watano hawajapewa ruhusu ya kuingia kwenye vituo vya kupigia kura vya shule ya Msingi Miembeni kwa kile anachodai hawatambuliki.
Akizungumza na Mwananchi, leo Jumapili Septemba 16, 2018, Faki amesema hafahamu kwa nini kitendo hicho kimejitokeza kwa sababu amefuata njia zinazotakiwa kuwapata mawakala hao.
“Tuna barua za mawakala, lakini wakifika katika vituo wanaambiwa hawatambuliki, nimeenda kituo kimoja baada ya kingine, toka saa 12 asubuhi nahangaika kuwatafutia vituo.
“Hii ni kwa chama cha CUF, vyama vingine mawakala wao wapo ndani ya vituo. Fomu zinazowatambulisha zipo, lakini wakionyesha kwa wahusika wanasema siyo kituo hiki wakatafute sehemu nyingine na wakifika huko wanaambiwa hivyohivyo,” amesema
Faki amesisitiza kuwa mawakala wake wote wana fomu za kopi na zile zenye uhalisia wanakuwa nazo wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi, lakini wakifika kituoni kulinganisha wahusika wanaelezwa fomu zao hazipo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Uhamasishaji wa CUF Vingunguti, Hussein Mahunda anasema, “Hapa tumepigwa bao la asubuhi mapema, hatuna chetu ila tulitambue tu. Mawakala wameshakataliwa unatarajia nini tena.”