Monduli. Mgombea ubunge wa Chadema, Yonas Laizer amesema hana matumaini ya ushindi wa ubunge jimbo la Monduli kutokana na uchaguzi kutawaliwa na kasoro nyingi.
Akizungumza na Mwananchi, Laizer baada ya kupiga kura katika vituo cha Losimongori, amesema uchaguzi umefanyika lakini amebaini njama za wazi za CCM kulazimisha ushindi.
Amesema mawakala zaidi ya 100 kati ya mawakala 256,hawakuwepo vituo vya kura. "Kuna mawakala wetu wamefukuzwa vituoni kwa sababu ambazo si sahihi, wengine wameambiwa hawana utambulisho, wengine wamepewa barua za uwakala wa udiwani na wengine wameshawishiwa," amesema
Amesema kuna maeneo amekuta wakala wakiwa wamefukuzwa na kujificha porini na wengine kutekwa," amesema.
Amesema katika mazingira ya aina hii hawezi kuwa muongo kuwa atashinda.
"Ambacho tunafanya sasa ni ku-document (kukusanya) taarifa zote na baadaye tutatoa taarifa rasmi," amesema.
Laizer pia ni diwani kata ya Lepurko.
Hata hivyo, msimamizi wa uchaguzi jimbo la Monduli, Stevin Ulaya amesema hana taarifa za mawakala kufukuzwa.
"Mimi natembelea vituo, sijaona mawakala waliofukuzwa na sijapokea malalamiko yoyote rasmi hadi sasa," amesema.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Arusha, Ramadhani Ng'azi amesema hana taarifa za wakala yeyote kutekwa na uchaguzi umekwenda kwa amani.