Dar es Salaam. Meya wa Manispaa ya Iringa, Alex Kimbe amepewa siku tano kujibu tuhuma zinazomkabili ikiwamo matumizi mabaya ya madaraka.
Hatua hiyo imefika baada ya wajumbe 19 wa Baraza la Madiwani la manispaa hiyo, kusaini maombi wakitaka kifanyike kikao maalum cha kujadili kumng’oa madarakani.
Kulingana na barua iliyosainiwa leo Jumatatu, Machi 2, 2020 na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, Hamid Njove meya huyo anatakiwa kuwasilisha utetezi wake kwenye ofisi za mkurugenzi huyo ndani ya siku tano kuanzia leo.
Miongoni mwa tuhuma zinazomkabili Kimbe ni matumizi mabaya ya madaraka ikiwamo kufanya maamuzi bila kuzingatia kanuni za kudumu za Halmashauri ya Manispaa ya Iringa.
Tuhuma nyingine ni matumizi mabaya ya rasilimali za halmashauri hiyo ikiwamo kutumia gari la halmashauri kwa matumizi yake binafsi.
Kulingana na barua inayosambaa kwenye makundi ya whatsapp, kanuni za kudumu za Halmashauri ya Manispaa ya Iringa za mwaka 2015, zinamwagiza mkurugenzi baada ya kupokea maombi ya tuhuma zinazomkabili meya, anatakiwa kupewa taarifa na kuandaa majibu ndani ya siku tano.
Pia Soma
- Mbunge wa tano CUF ahamia CCM
- Majaliwa aagiza mweka hazina Wilaya ya Mkinga achunguzwe
- Lema adai kuitwa polisi Arusha leo
Barua hiyo inafafanua kuwa timu ya uchunguzi baada ya kukamilisha kazi yao na kuisasilisha taarifa hiyo kwa mkuu wa mkoa, kiongozi huyo atairejesha kwa mkurugenzi wa manispaa ndai ya siku 14 kisha itapelekwa kwenye baraza la madiwani kwa ajili ya uamuzi wa tuhuma husika.
“Hivyo nakuomba upokee tuhuma zinazokukabili na unatakiwa kujibu ndani ya siku tano tangu tarehe ya barua hii na majibu ya utetezi yafike ofisi ya mkurugenzi,” inasema sehemu ya Barua.
Ofisa Habari wa Manispaa ya Iringa, Sima Bingileki amekiri kuwa barua hiyo imetoka halmashauri.
Akizungumza na Mwananchi, Kimbe amedai kupata taarifa za kuwapo barua hiyo na kwamba, ameelekea Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kupata ufafanuzi.
“Baada ya saa moja nitaeleza, naenda halmashauri muda huu,” amesema Kimbe.