Dar es Salaam. Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa amesema vyama vinavyounda Ukawa vinaweza kuishinda CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, ikiwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) itakuwa huru na kutenda haki.
Mchungaji Msigwa ametoa kauli hiyo leo jioni Jumapili Agosti 5, 2018 katika kipindi cha Siasa za Kanda kinachorushwa na kituo cha televisheni cha KTN cha nchini Kenya.
Mada kuu katika kipindi hicho ilikuwa ni kujadili hali ya siasa za upinzani barani Afrika huku wachangiaji wa mada hiyo wakiunganishwa kutoka Zambia, Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC), Zimbabwe, Kenya, Uganda na Tanzania.
“Kumekuwa na nguvu isiyo ya kawaida kugandamiza vyama vya upinzani, wasimamizi ambao wanatakiwa kuwa neutral (kutokuwa na upande) wameteuliwa na mtu kutoka chama kilichopo madarakani, kwa hiyo inakuwa ngumu,“amesema.
“Sisi tuna nguvu ya kuishinda Serikali iliyopo madarakani na tukachukua nchi.”
Amesema hilo litasukumwa zaidi na uwanja sawa wa kufanya siasa pamoja na kuwa na Katiba nzuri na NEC huru.
Mchungaji Msigwa alitoa kauli hiyo baada ya kuulizwa swali na mtangazaji wa kipindi hicho kuhusu ugumu wa wapinzani nchini kuing’oa CCM madarakani, akihusisha suala hilo na wapinzani kukosa uimara.